Main Title

source : Parstoday
Ijumaa

6 Agosti 2021

22:52:44
1167124

Sera za kigeni za serikali ya Raeisi; ushirikiano erevu na ulimwengu, mtazamo maalumu kwa majirani

Rais wa nane wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amebainisha katika hotuba yake ya kwanza mara baada ya kuapishwa kuhusiana na utendaji wa serikali mpya ya Iran kuhusiana na sera za kigeni kwa ajili ya kudhamini maslahi ya kitaifa katika uga wa kieneo na kimataifa.

Shirika la habari la Ahlubayt (as)ABNA: Ibrahim Raeisi aliapishwa alasiri ya jana Alkhamisi katika ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mbele ya maafisa, viongozi, shakhsia wa kisiasa kutoka mataifa mbalimbali ya dunia na wawakilishi wa jumuiya za kieneo na kimataifa na kusisitiza kwamba: Serikali mpya nchini Iran itatumia nyenzo zote za nguvu za kitaifa kama “udiplomasia na ushirikiano erevu” na ulimwengu kwa ajili ya kudhamini maslahi ya kitaifa ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Rais wa nane wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amebainisha masuala muhimu zaidi na vipaumbele  vya sera za kigeni za serikali yake akiwa na mtazamo maalumu kwa nchi jirani na za kieneo. Aidha amebainisha kuwa, lengo la kuimarisha nguvu ya Iran ni  kutumika nguvu hiyo ya Jamhuri ya Kiislamu kwa ajili ya kuleta amani na usalama wa eneo.

Baada ya ushindi wa Mpinduzi ya Kiislamu yaliyotokea mwaka 1979 kwa uongozi wa busara wa Imam Ruhullah Khomeini, kipaumbele muhimu kabisa katika siasa za kigeni za Tehran ni kuboresha na kupanua uhusiano na nchi jirani; na taifa hili linaaamini kuwa, usalama na uthabiti wa majirani na nchi za eneo ni usakama na uthabiti wake.

Iran inaamini kuwa, ushirikiano na mazungumzo ya kieneo ndio nguvu kuu, muhimu na ya kimsingi kwa ajili ya kufikia malengo ya amani na utulivu wa eneo. Katika fremu hii, Rais mpya wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kubainisha sera zake za kigeni ameeleza kuwa, anayanyooshea mkono wa urafiki mataifa jirani na ya eneo hili.

Tajiriba ya miaka kumi ya hivi karibuni ya matukio ya eneo la Asia Magharibi imeonyesha wazi na bayana kwamba, uwezo wa kieneo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran umekuwa kwa ajili ya kuhudumia amani, usalama na uthabiti wa nchi za mataifa ya eneo. Himaya na uungaji mkono wa Iran kwa mataifa ya Iraq na Syria katika kupambana na kundi la kigaidi la Daesh na kulisambaratisha kundi hilo ni mfano wa wazi wa Iran kutumia uwezo wake wa kieneo kwa ajili ya kuunga mkono mataifa na tawala za kieneo katika kukabiliana na vitisho kutoka nje ya eneo hili.

Katika uga wa kiulinzi, kijeshi, kiuchumi, kielimu na kiviwanda, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ina uwezo mkubwa na uwezo huu upo kwa ajili ya kuhudumia majirani na nchi za eneo hili, na katu uwezo huo hauko dhidi ya mataifa hayo. Kama alivyosema na kusisitiza wazi Rais mpya wa Iran mbele ya viongozi mbalimbali jirani na ya kieneo walioshiriki katika hafla ya kuapishwa kwake ni kuwa, uwezo wa kieneo wa Iran utatumika kwa ajili ya kukabiliana na madoja ajinabi na mabeberu.

Katika mazingira kama haya; Iran daima imekuwa ikiamini na kusisitiza kwamba, njia ya kupatiwa ufumbuzi migogoro ya eneo ni mazungumzo ya ndani ya eneo hili na kwamba, uwepo wa madola ya kigeni ni kwa madhara kwa uthabiti na usalama wa eneo. Ushirikiano na mahusiano makubwa ya Iran na majirani pamoja na nchi za eneo ni kwa maslahi ya pande mbili na kama hili litafanyika vyema, basi nyenzo za vikwazo havitaweza kuwa na taathira hasi kwa maslahi ya kiuchumi na kisiasa ya mataifa haya.

Iran inatambua kuwa, ustawi na maendeleo ya nchi  jirani  ni kwa maslahi yake na ya eneo, kwani kupata nguvu nchi za eneo na majirani ni kwa maslahi ya kuimarisha mizizi ya usalama na uthabiti katika eneo la Asia Magharibi.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na nchi jirani na za eneo la Asia Magharibi zina mambo mengi zinazoshirikiana, na Rais Ibrahim Raeisi kwa kuzingatia nukta hii muhimu akibainisha sera zake za kigeni amesisitiza juu ya kupanuliwa na kustawishwa uhusiano na ushirikiano na majirani pamoja na nchi za eneo hili.

342/