Main Title

source : ABNA24
Ijumaa

29 Aprili 2022

14:20:51
1253040

Maandamano ya Siku ya Quds kote Iran, Kiongozi Muadhamu kuhutubia umma

Maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds yanafanyika kote nchini Iran ambapo idadi kubwa ya wananchi wamejitokeza kutangaza uungaji mkono wao kwa harakati za ukombozi wa Palestina sambama na kulaani jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel.

Leo Ijumaa tarehe 29 Aprili inayosadifiana na tarehe 27 Ramadhani 1443 Hijria Qamaria, ni Siku ya Kimataifa ya Quds. 

Shirika la habari la Ahlubayt (as)ABNA: Imam Ruhullah Khomeini (Mwenyezi Mungu Amrehemu) Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran  aliitangaza Ijumaa ya mwisho ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani kuwa Siku ya Kimataifa ya Quds ili kuibakisha hai kadhia muhimu ya Palestina na kupawa Waislamu duniani kote fursa ya kutangaza mshikamano wao na Wapalestina sambamba na kukusanya nguvu kwa ajili ya kuikomboa Quds Tukufu kutoka kwenye makucha ya Wazayuni maghasibu.

Maandamano ya Siku ya Kimataifa ya Quds nchini Iran yanafanyika kwa kushiriki wananchi katika maandamano baada ya kufanyika kwa miaka miwili kupitia misafara ya magari na kupitia intaneti kutokana na janga la corona.

Mbali na hapa nchini Iran, maandamano pia yamekuwa yakifanyika katika maeneo mbali mbali kote duniani na yataendelea wikiendi hii pia hasa katika nchi za Magharibi.

Wananchi wa Iran wanaoshiriki katika maandamano ya leo wamesikika wakipiga nara za kuunga mkono taifa la Palestina linalodhulumiwa huku pia wakipiga nara za 'Mauti Kwa Israel', na 'Mauti kwa Marekani' sambamba na kulaani tawala za Kiarabu ambazo zimewasaliti Wapalestina kwa kuanzisha uhusiano na utawala wa Kizayuni wa Israel.   

Wakati huo huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei leo atahutubu kwa njia ya moja kwa moja kupitia televisheni kwa munasaba wa Siku ya Kimataifa ya Quds.

Kwa mujibu wa tovuti ya Kiongozi Muadhamu , hotuba hiyo itaanza leo Ijumaa saa 10 jioni kwa saa za hapa Tehran sawa na saa nane unusu kwa saa za Afrika Mashariki na itarushwa hewani mubashara kupitia radio na televisheni za kimataifa za Shirika la Utangazaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kama vile Press TV, Al Alam, Al Kauthar, Hispan TV na Iran Press.



342/