Ripoti ya shirika la habari la Ahlul Bayt(as)- ABNA - Televisheni ya al Alam imemnukuu Abdul Salam Hanafi akisema hayo na kusisisitiza kuwa, maadui wa Uislamu na Afghanistan hawapaswi kupewa fursa kabisa ya kujipenyeza kwenye jamii yetu na kueneza vita vya kikabila na kimadhehebu.
Aidha amesema kama ninavyomnukuu: Sisi si Masuni na si Mashia, bali sote ni sawa na mwili mmoja yaani sote ni Waislamu. Ni sawa kwamba sisi tunamfuata Imam Abu Hanifa lakini tunamuheshimu pia Imam Jaafar al Sadiq AS.
Naibu Waziri Mkuu wa serikali ya Taliban vile vile amesema: Wanaomfuata Imam Jaafar al Sadiq AS ni ndugu zetu kwani na wao pia wanawaheshimu Imam Abu Hanifa, Imam Shafi, Imam Malik na Imam Ahmad ibn Hambal na wanavyuoni wengine wakubwa.
Amesisitiza tena kwa kusema: Sisi sote ni mwili mmoja na sote tunaishi ndani ya nchi moja. Sisi sote ni Waislamu. Sote ni Waafghani, nchi yetu ni moja. Kwa karne nyingi tunaishi hapa kwa pamoja kiudugu. Katika siku za usoni pia Insha'Allah tutaendelea kuwa kitu kimoja na tutasali ndani ya msikiti moja, tutaishi kwenye mtaa mmoja na katika mji mmoja bila ya wasiwasi wowote.
Naibu Waziri Mkuu huyo wa serikali ya Taliban ya Afghanistan pia amesema, hakuna adui yeyote anayeweza kutugombanisha na kututenganisha. Adui yeyote hana ruhusa ya kufanya hivyo.
Hivi karibu pia Abdul Salam Hanafi alionana na familia za Waislamu waliouawa shahidi katika Msikiti wa Mashia huko Mazar Sharif na kulaani mashambulo ya kigaidi. Alisema, Waafghani wote wako sawa hakuna tofauti baina ya Mashia na Masuni, wote ni kitu kimoja.
342/