Kuibuka ghasia na machuko hivi karibuni hapa nchini kwa kisingizio cha kifo cha Mahsa Amini kwa mara nyingine tena kumewapelekea maadui wa nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kustafidi na matukio hayo kama fursa ya kuingilia masuala ya ndani ya Iran na pia kuchochea pakubwa ghasia nchini.
Kuhusiana na suala hilo, Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz jana alituma ujumbe katika ukurasa wake wa twitter akisema: wiki ijayo ataunga mkono duru mpya ya vikwazo vya Umoja wa Ulaya dhidi ya Iran.
Nasser Kan'ani Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran leo ameeleza kuwa, baadhi ya nchi zinazodai kutetea haki za binadamu zimesahau rekodi zao chafu mkabala wa wananchi wa Iran kwa uungaji mkono wao wa kidhalimu na kinyume na ubinadamu kwa utawala wa Saddam; na wakati huo huo kuiwekea Iran vikwazo vya kidhalimu baada ya Marekani kujitoa kwa upande mmoja katika mapatano ya JCPOA. Amesema, nchi hizo aidha zimenyamazia kimya hujuma za kigaidi za Daesh ambapo tukio la karibuni likiwa ni shambulio dhidi ya Haram takatifu la Shah Cheragh huku zikitumia suala la haki za binadamu kama msingi wa michezo ya kisiasa.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran aidha amesisitiza tena kuwa kuvuruga uhusiano wa kihistoria kuna madhara ya muda mrefu na kwamba Iran ina orodha ndefu ya matakwa yake ya haki za binadamu kwa Ujerumani; kwa msingi huo ni Ujerumani ndiyo inayopasa kufafanua kwa uwazi yaliyopita.
Kan'ani kwa mara nyingine tena amewashauri viongozi wa Ujerumani kurejesha mantiki katika anga ya uhusiano ili kuzuia kuvurugika zaidi maingiliano kati yao na kwamba kuheshimiana pande mbili ni njia pekee ya kuendeleza ushirikiano wa kudumu.
342/