Main Title

source : Parstoday
Ijumaa

18 Novemba 2022

19:14:15
1324321

Moto waua watu 21 Ukanda wa Gaza, Mamlaka ya Ndani yatangaza maombolezo ya umma

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Ukanda wa Gaza imetangaza habari ya kufariki dunia watu wote waliokuwa katika jengo la ghorofa lililoteketea kwa moto katika kambi ya Jabalia kaskazini mwa Ukanda wa Gaza, huku Jeshi la Ulinzi la Wananchi likieleza kuwa wafanyakazi wake wameopoa miili 21 ya waliofariki dunia kutokana na moto huo.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya serikali ya Gaza, Iyad Al-Bazm, amethibitisha, katika taarifa yake, kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha "kuwapo kwa petroli iliyokuwa imehifadhiwa ndani ya nyumba hiyo, ambayo ilisababisha mlipuko mkubwa wa moto na kuua idadi hiyo ya watu."

Al-Bazm amesema kamati maalumu imeundwa ili kuchunguza pande zote kuhusu moto huo.

Kwa upande wake mkurugenzi wa magari ya kubebea wagonjwa katika Hospitali ya Indonesia iliyopo Jabalia, Salah Abu Laila amesema miili 20 iliyoungua imepelekwa hospitalini hapo baada ya kuungua kwa jengo la familia ya Abu Raya mjini Jabalia na kueleza kuwa watoto wasiopungua 7 ni miongoni mwa waliofariki dunia katika tukio hilo.

Mwandishi wa televisheni ya Al-Jazeera katika Ukanda wa Gaza amenukuu chanzo cha matibabu kikisema kuwa watu 21 wa familia moja wamefariki dunia katika moto huo uliozuka jana Alhamisi katika jengo la makazi kwenye eneo la Tel Zaatar katika kambi ya Jabalia kaskazini mwa Ukanda wa Gaza.

Mashuhuda wa tukio hilo wameeleza kuwa walisikia kelele za watu lakini hawakuweza kuwafikia wahanga ili kutoa msaada kutokana na kukithiri kwa moto huo.

Kufuatia moto huo, Mamlaka ya Ndani ya Palestina imetangaza maombolezo ya umma leo Ijumaa.

342/