Shirika la Habari la Fars limelinukuu, gazeti la Kizayuni "Yedioth Aharonoth" likiripoti habari hiyo ikiwa ni mara ya kwanza katika historia ya siasa za Tel Aviv, kuchapishwa habari kuhusu kuhusika wanasiasa wa utawala huo pandikizi katika mashambulizi ya mabomu ya mwaka 1954 nchini Misri, ambayo hapo awali ilikuwa ni marufuku kutangaza habari kama hiyo.
Gazeti hili limemnukuu "Benjamin Gibli" aliyekuwa mkuu wa idara ya kijasusi ya kijeshi ya utawala wa Kizayuni (Aman) katika miaka ya khamsini ya karne iliyopita akikiri kwamba waziri wa vita wa wakati huo wa Israel Pinhas Lavon aliamuru yeye mwenyewe kuanzishwa mtandao wa kijasusi unaoundwa na Wayahudi wa Misri ili kufanya mashambulizi ya mabomu huko Misri.
Katika wasifu wake binafsi ambao gazeti la Yedioth Aharonoth, ndilo pekee lililopewa haki ya kuuchapisha, Gibli ameandika kwamba Lavon aliniacha "nitafunwe na mbwa" baada ya kufichuka mtandao wetu wa kijasusi huko Misri.
Vyombo vya habari vya Kizayuni vimeanza kufichua sehemu za wasifu wa jenerali huyo jasusi wa utawala wa Kizayuni baada ya kupita miaka 14 tangu kuangamia kwake.
Suala hili linahusiana na operesheni ya kijasusi ya mwaka 1954 iliyoongozwa na Kitengo cha 131 cha shirika la kijasusi la Israel "Aman" na lengo lake lilikuwa ni kuripua majengo ya raia na majengo ya Waingereza na Wamarekani huko Misri kwa kutumia Mayahudi wa Misri.
342/