Jimbo la Tigray kaskazini mwa Ethiopia linashuhudia upungufu mkubwa wa chakula kwa karibu miaka miwili sasa na hali inazidi kuwa mbaya siku baada ya siku.
Lakini hali imekua mbaya zaidi tangu mashirika ya misaada ya dharura kusitisha kwa muda ugawaji wa chakula kutokana na tuhuma za utumiaji mbaya wa misaada ya chakula inayotolewa.
Mashirika ya misaada ya dharura yalisitisha mipango yao ya kupeleka chakula kwa watu wanaokabiliwa na nja katika jimbo la Tigray baada ya ripoti ya wakaguzi wa Umoja wa Maraifa kueleza kwamba chakula cha msaada kinapelekwa kwa wanajeshi na wala si watu waliokusudiwa.
Wakati huo huo, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limesema kwamba ukame unaoendelea katika maeneo kadhaa ya Ethiopia umeua karibu mifugo milioni 6.8.
Katika ripoti yake mpya ya mpango wa kukabiliana na hali ya kibinadamu wa Ethiopia, FAO ilisema hasara kubwa ya mifugo ilitokea katika mikoa ya Oromia, Somali na Kusini mwa nchi hiyo. Athari hizi za ukame pia zimeingia katika uzalishaji wa mazao, upotevu wa mapato, viwango vya juu vya utapiamlo na uhaba wa chakula.
Shirika hilo la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji limesema hayo katika maelezo yake ya muhtasari ya hivi karibuni na kuongeza kuwa, jamii za maeneo ya kusini na mashariki mwa Ethiopia zinakabiliwa na ukame mkubwa kufuatia misimu mitano ya kukosekana mvua za kutosha.
Takriban wakimbizi wa ndani milioni 3 waliorodheshwa nchini Ethiopia mwaka wa 2022, huku hatari za watu wengi zaidi kuhama makazi mwaka huu wa 2023 zikitabiriwa kuwa kubwa zaidi.
342/