Main Title

source : Parstoday
Ijumaa

1 Septemba 2023

20:21:38
1390512

Kuendelea kugunduliwa makaburi ya halaiki ya watoto asili wa Canada

Katika miaka ya hivi karibuni, kugunduliwa makaburi ya halaiki na miili ya mamia ya watoto wenyeji waliozikwa kwa siri nchini Canada kumefichua mauaji ya kutisha na ubaguzi wa rangi uliofanywa dhidi ya wenyeji wa nchi hiyo, suala ambalo limewashangaza wanaharakati wengi wa kutetea haki za kiraia, viongozi wa kisiasa na wawakilishi wa maoni ya umma ndani na nje ya mipaka ya Canada.

Ugunduzi wa makaburi hayo ungali unaendelea kiasi kwamba katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, zaidi ya makaburi 1,300 ya watoto yamegunduliwa karibu na baadhi ya taasisi za kielimu za makanisa ambazo zilikuwa sehemu ya mfumo wa elimu kwa ajili ya watoto wenyeji wa nchi hiyo. Kuhusiana na suala hilo, siku ya Jumatano moja ya makabila ya wachache ya wazawa asilia wa Canada yanayoishi magharibi mwa nchi hiyo lilitangaza kugunduliwa kwa kaburi la umati la watoto wapatao mia moja katika eneo hilo.

Kabila hilo la The English River First Nation limesema kwamba kilichogunduliwa kinahuzunisha sana. Kufikia sasa, makaburi 93 ambayo hayana alama yoyote yakiwemo ya watoto 79 na watoto wachanga 14 yamegunduliwa katika nchi hiyo.

Makaburi mapya yamegunduliwa kufuatia utafiti uliofanywa karibu na shule ya bweni ya wenyeji asilia inayoitwa Beauval katika eneo la Saskatchewan, Canada. Kwa mujibu wa Chuo Kikuu cha Regina, majengo ya shule hiyo yaliharibiwa na wakaazi baada ya kufungwa mnamo 1995.