Main Title

source : Parstoday
Alhamisi

7 Septemba 2023

15:09:31
1391901

UN yatiwa wasiwasi na Marekani kuipelekea Ukraine risasi zenye urani hafifu

Umoja wa Mataifa umesema umetiwa wasiwasi na tangazo la Wizara ya Ulinzi ya Marekani, kwamba Washington itaipelekea Ukraine risasi zenye madini ya urani iliyohafifishwa.

Wizara ya Ulinzi ya Marekani (Pentagon) ilitangaza jana Jumatano kwamba: Marekani itaipa Ukraine risasi za mizinga zenye madini ya urani hafifu ikiwa ni sehemu ya shehena mpya ya msaada wenye thamani ya dola milioni 175.   Baada ya kuthibitishwa ripoti za kutumwa shehena ya risasi za vifaru zenye urani hafifu, Farhan Haq, naibu msemaji wa Umoja wa Mataifa alitangaza hapo jana kuwa, Umoja wa Mataifa umekuwa na wasiwasi kila mara juu ya kutumiwa risasi zenye urani hafifu katika sehemu yoyote ya dunia.   Haq alisema: "wasiwasi wetu kuhusu utumiwaji wa urani hafifu katika sehemu yoyote duniani ni thabiti na ungali upo palepale".   Kabla ya hapo, shirika la habari la Reuters iliripoti kuwa kwa mara ya kwanza, utawala wa Joe Biden utaipatia Ukraine risasi zenye urani iliyohafifishwa.  

Utumiaji wa risasi zenye madini ya urani hafifu ni miongoni mwa masuala yanayopigiwa kelele; na wapinzani wake, ukiwemo Muungano wa Kimataifa wa Kupiga Marufuku Silaha zenye Urani, wametangaza kuwa aina hiyo ya silaha ni hatari na husababisha saratani au kuzaliwa watoto wenye ulemavu. 

Marekani ilitumia kwa wingi risasi zenye urani hafifu katika vita vya Ghuba ya Uajemi kwenye miaka ya 1990 na 2003. Mnamo mwaka 1999, shirika la kijeshi la NATO, nalo pia lilitumia silaha hizo angamizi katika mashambulio dhidi ya Yugoslavia.   Uzoefu wa vita umeonyesha kuwa, kama yalivyo mabomu ya vishada, risasi zenye urani iliyohafifishwa huua zaidi raia kuliko askari.../

 342/