Shirika la Umoja wa Mataifa la UN WOMEN linalohusika na masuala
ya wanawake na UNDESA ambayo ni Idara ya Umoja wa Mataifa ya uchumi na
kijamii, yamezindua ripoti yao ya kila mwaka inayotathimini namna
malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs yanavyotekelezwa kwa kuzingatia
usawa wa kijinsia.
Utafiti wa mwaka huu ulihusisha nchi 116, na pamoja na mambo mengine uliweka mkazo kwa wanawake wazee ambapo ripoti ilionyesha kuwa kundi hilo ndani ya jamii linakabiliwa na viwango vikubwa si tu vya umasikini na kutokuwa na pensheni, bali pia ukatili, ikilinganishwa na wanaume wazee.
Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa UN WOMEN Bi.Sarah Hendriks amesema ripoti ya mwaka huu ni wito mkubwa wa kuchukua hatua kwa kuzingatia kuwa, utelekezaji wa SDGs umefika nusu ya muda uliopangwa kabla ya kufikia kilele hapo mwaka 2030.
Imeelezwa katika ripoti hiyo ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa kwamba licha ya suala la usawa wa kijinsia kupigiwa upatu kila kwenye majukwaa makubwa hususan ya wafanya maamuzi, pengo la kijinsia katika madaraka na nyadhifa za uongozi bado limekita mizizi, na kwa kasi ya sasa ya maendeleo, ripoti imesema, kizazi kijacho cha wanawake kitaendelea kutumia wastani wa saa 2.3 zaidi kwa kila siku bila ujira wakati wakifanya kazi za nyumbani kuliko wanaume.
Ripoti hiyo pia inajumuisha wito wa kuwa na mtazamo jumuishi na wa kiujumla, ushirikiano mkubwa kati ya wadau, ufadhili endelevu, na hatua za kisera za kushughulikia ufa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake na wasichana duniani kote; ikihitimisha kwamba kushindwa kuweka kipaumbele kwa usawa wa kijinsia sasa hivi kunaweza kuhatarisha Ajenda nzima ya 2030 ya SDGs.../
342/