Kila
siku umati mkubwa wa wananchi wa Niger umekuwa ukijumuika mbele ya
kambi ya kijeshi ya Ufaransa kufutia hukumu iliyotolewa na serikali ya
kijeshi ya kuondoka wanajeshi na balozi wa Ufaransa nchini Niger.
Kwa mujibu wa ripoti ya shirika la habari la Iranpress mjini Niamey, jana Jumapili makamanda wakuu wa jeshi la Niger pia walijiunga na mujumuiko huo jambo ambalo lilikaribishwa na wananchi. Shirika la Iranpress limnukuu vyombo rasmi kwamba Ufaransa imetangaza mpango wa kuwaondoa wanajeshi wake nchini humo sambamba na hatua hiyo ya jeshi la nchi hiyo.
Ripoti zinasema kwa kuzingatia umati mkubwa unaojumuika kila siku mbele ya kambi hiyo inatarajiwa kuwa wanajeshi hao wataondoka nchini humo hivi karibuni. Mmoja wa makamanda waandamizi wa jeshi la Niger alisisitiza katika mazungumzo yake mbele ya umati mkubwa ulazima wa kuondoka haraka wanajeshi wa Ufaransa nchini humo.
Inasemekana kuwa matamshi hayo yalikaribishwa kwa shangwe na wananchi wa Niger.
Kikosi cha Gadi ya Rais wa Serikali ya Niger tarehe 26 Juni 2023 kilimuondoa madarakani Muhammad Bozoum rais wa Jamhuri wa Niger kwa tuhuma za ufisadi, kushirikiana na nchi za Magharibi na kutoshughulikia umasikini wa wananchi. Viongozi wa kikosi hicho wamekataa ombi la Umoja wa Mataifa, nchi za Magharibi na Jumuia ya Kiuchumi ya Nchi za Magharibi mwa Afrika, ECOWAS, la kumrejesha madarakani kiongozi huyo.
342/