Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Iraq, Madluh Muhammad, ambaye ni maarufu kwa jina la Madlulah, ajuza wa Kiiraq aliyeishi umri mrefu zaidi, amefariki dunia leo Alkhamisi katika eneo la al-Islah, lililoko mashariki mwa mji wa Nasiriyah kutokana na maradhi. Madlulah alizaliwa Julai Mosi, mwaka 1885 na amefariki dunia baada ya miaka 138 kutokana na kusibiwa na maradhi. Kwa mujibu wa cheti cha uthibitisho wa kifo chake, yeye ndiye mtu mzee zaidi nchini Iraq na pengine duniani kote. Kulingana na ripoti za vyombo vya habari vya Iraq, Madluh Muhammad aliolewa mara tatu maishani mwake na alikuwa na mtoto mmoja tu wa kiume, ambaye alikuwa mwanajeshi na aliuawa miaka kadhaa nyuma akiwa kazini katika mapigano yaliyohusisha vikosi vya usalama vya Iraq. Jamaa za ajuza huyo wamesema: Madluh Muhammad aliishi maisha ya kawaida tu siku chache kabla ya kifo chake, lakini katika siku za hivi karibuni alisumbuliwa na matatizo makubwa ya maradhi.../
342/