Main Title

source : Parstoday
Ijumaa

3 Novemba 2023

17:11:09
1408104

Sayyid Nasrullah: Machaguo yote dhidi ya Israel yapo mezani

Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon amesema machaguo yote dhidi ya utawala haramu wa Israel yapo mezani, huku akiuasa utawala huo wa Kizayuni usitishe mara moja uvamizi na mashambulizi yake ya kinyama dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza.

Katika hotuba yake iliyorushwa kwa njia ya televisheni leo Ijumaa, Sayyid Hassan Nasrullah amesema Hizbullah iko tayari kwa ajili ya chochote, na kwamba yeyote mwenye azma ya kuzuia vita vya kieneo, basi aharakishe kusimamisha uvamizi wa Israel dhidi ya Gaza.

Ameashiria hatua ya Marekani ya kutuma manowari za kijeshi katika eneo la Asia Magharibi na kusisitiza kuwa: Harakati ya Hizbullah haiogopi wala haibabaishwi na kitu chochote.

Sayyid Hassan Nasrullah amebainisha kuwa, Operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa ya Oktoba 7 iliratibiwa na kutekelezwa kwa asilimia 100 na Wapalestina wenyewe, huku akipuuzilia mbali madai kuwa ilipanga na mataifa ya eneo.

Ameeleza kuwa: Usiri wa hali ya juu wa operesheni hiyo ndiyo sababu kuu ya kufanikiwa kwake. Sayyid Nasrullah ameongeza kuwa, Kimbunga cha al-Aqsa kimeisababishia Israel zilzala na mtetemeko mkubwa wa kiusalama, kijeshi, kisaikolojia na kiari. Amesema tetemeko hilo la kistatajia litaacha athari nyingi hasi kwa utawala wa Kizayuni hivi sasa na hata baadaye.

Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon amebainisha kuwa: Operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa kimefichua udhaifu na idhilali ya Israel, na kwamba utawala huo wa Kizayuni ni kwa hakika ni dhaifu zaidi ya utandu wa buibui.Amesema Hizbullah iliingia katika vita dhidi ya Israel mnamo Oktoba 8, siku moja baada ya makundi ya muqawama ya palestina kufanya Operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa.

Kiongozi huyo wa muqawama wa Lebanon amesema kufikia wanamapambano 57 wa Hizbullah wameuawa shahidi kwenye operesheni dhidi ya Wazayuni.

Sayyid Nasrullah amesema kuna uwezekano vita hivyo vikapanuka kutoka upande wa Lebanon na vitageuka na kuwa vita vikubwa vya kieneo.

Amewapongeza wanamapambano wa Iraq na Yemen ambao pia wamejitosa kwenye vita hivi vitakatifu vya kuwahami na kuwalinda wananchi madhulumu wa Palestina. 



342/