Shirika la habari la IRNA limeripoti leo kuwa, Manu Pineda, mwakilishi wa Uhispania katika Bunge la Ulaya na mkuu wa kamati ya uhusiano wa Umoja wa Ulaya na Palestina, ambaye amelaani mara kadhaa jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza na uungaji mkono wa nchi za Magharibi kwa mauaji ya kimbari yanayofanywa na utawala huo katika eneo hilo amesema: "hatuwezi kuacha jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina wanaoishi katika Ukanda wa Gaza zipite bila wahusika kuadhibiwa. Tuna wajibu wa kumburuza Benjamin Netanyahu, waziri mkuu wa utawala wa Wazayuni na washirika wake wengine kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu."
Katika miezi ya hivi karibuni, na kufuatia kushadidi mashambulio ya utawala wa Kizayuni dhidi ya Ukanda wa Gaza, wabunge wengi wa Bunge la Ulaya akiwemo Mark Butenga wa Ubelgiji na Mick Wallace wa Ireland wamekuwa wamekosoa mara kadhaa jinai na mashambulio ya utawala wa Kizayuni dhidi ya Ukanda wa Gaza na kutoa wito wa kusitishwa mapigano katika eneo hilo.
Kuanzia tarehe 7 Oktoba, na kwa uungaji mkono kamili wa nchi za Magharibi, utawala wa Kizayuni ulianzisha hujuma na mashambulio makubwa na mauaji ya kinyama katika Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan dhidi ya watu madhulumu na wasio na ulinzi wa Palestina. Tangu yalipoanza mashambulio hayo ya utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Gaza, Wapalestina wasiopungua 19,453 ambao wengi wao ni wanawake na watoto wameuawa shahidi na wengine 52,286 wamejeruhiwa.../
342/