Kwa mujibu wa shirika la habari la FARS, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anaongoza ujumbe wa ngazi za juu wa kisiasa wa nchi yake kutembelea nchi za eneo hili la Asia Magharibi na safari ya ujumbe huo wa Iran imeanzia Beirut Lebanon. Akiwa mjini Beirut, Hossein Amir-Abdollahian ameonana na viongozi wa makundi ya muqawama ya Palestina kama ambavyo ameonana pia na Sayyid Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon.
Katika mazungumzo yake na wakuu wa makundi ya muqawama ya Palestina; mazungumzo ambayo yamehudhuriwa pia na Ziyad al Nakhalah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Jihadul Islami, Usama Hamdan, mmoja wa viongozi wakuu wa harakati ya HAMAS pamoja na Jamil Mazhar, Naibu Katibu Mkuu wa Harakati ya Wananchi ya Ukombozi wa Palestina, pande hizo zimejadiliana matukio ya karibuni kabisa kwenye medani za mapambano na katika masuala ya kisiasa na kusisitiza kuwa matunda ya kusimama imara makundi ya muqawama na wananchi wa Palestina hasa huko Ghaza ni pamoja na kujitokeza kwa uwazi zaidi ushindi wa taifa la Palestina katika kila upande.
Amma katika mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran na Sayyid Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu huyo wa Hizbullah ya Lebanon amesema kuwa, ni jambo lisilo na chembe ya shaka kwamba, ushindi ni wa taifa la Palestina na kambi ya muqawama. Amesisitiza kuwa, miongozo ya busara na yenye thamani kubwa ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei kuhusu hali ya Ghaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan hivi sasa, ni miongozo ya kipekee kabisa.
Ujumbe huo wa Iran untararajiwa pia kutembelea Syria na Qatar katika juhudi za Jamhuri ya Kiislamu za kutatua kwa njia za amani matatizo mbalimbali yaliyopo kwenye eneo hili.
342/