Main Title

source : Parstoday
Jumatano

21 Februari 2024

12:51:08
1439474

Walimwengu wailaani US kwa kutumia veto kuzuia usitishaji vita Gaza

Mataifa na mashirika mbali mbali ya kimataifa yamelaani vikali hatua ya Marekani ya kutumia kura yake ya turufu kupinga rasimu ya azimio iliyowasilishwa na Algeria katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, la kutaka kusitishwa mara moja mapigano katika Ukanda wa Gaza.

Baraza la Uhusiano wa Kiislamu nchini Marekani (CAIR) limesema hatua ya Marekani ya kukataa kusitishwa mara moja mapigano huko Gaza kwa kulipigia kura ya veto azimio hilo ni ya fedheha, huku likimtaka Rais Joe Biden aache kujifanya kuwa wakili mtetezi wa Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala haramu wa Israel.

Mkurugenzi Mkuu wa CAIR, Nihad Awad amenukuliwa na kanali ya al-Jazeera akisema kuwa, kitendo hicho cha US kwa mara nyingine tena kimeonyesha ushiriki kamili wa Washington katika jinai na uhalifu unaofanywa na utawala ghasibu wa Israel.

Katika kikao hicho cha jana, wawakilishi wa nchi 13 kati ya 15 wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa walipiga kura kuunga mkono azimio hilo la kusitishwa vita Ukanda wa Gaza. Marekani ilipiga kura ya veto dhidi ya azimio hilo huku mshirika wake, Uingereza, ikijizuia kupiga kura.

Hii ni mara ya tatu kwa Marekani kutumia kura yake ya veto katika Baraza la Usalama kupinga azimio la kusitishwa vita vya maangamizi ya kizazi vinavyoendelea kufanya na utawala wa Kizayuni wa Israel katika Ukanda wa Gaza tokea Oktoba 7, 2023.

Jason Lee, Mkurugenzi wa shirika la misaada ya kibinadamu la Save the Children katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu amelaani hatua hiyo ya US na kusema kuwa, taasisi hiyo imeshtushwa na hatua hii mpya ya kutamausha ambayo inaashiria kufeli kwa jamii ya kimataifa. 

342/