Takriban Wapalestina 31,000 wameuawa shahidi na wengine zaidi ya 72,000 kujeruhiwa wengi wao wakiwa wanawake na watoto katika mashambulizi ya jeshi la Israel kwenye Ukanda wa Ghaza tokea kuanza operesheni ya Kimbunga cha al Aqsa tarehe 7 Oktoba 2023.
Kuhusiana na hilo, Rais Gabriel Borich wa Chile amesisitiza, katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari na Pedro Sanchez Waziri Mkuu wa Uhispania huko Santiago, mji mkuu wa nchi hiyo, kwamba Chile inaunga mkono usitishwaji vita huko Ghaza haraka iwezekanavyo na kuongeza kuwa yanayoendelea Ghaza hayakubaliki kabisa.
Katika mkutano huo wa pamoja na waandishi wa habari, Pedro Sanchez Waziri Mkuu wa Uhispania sambamba na kulaani mashambulizi ya utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi wasiokuwa na hatia wa Ghaza amesema: 'Ni jambo lisilokubalika kabisa kwa Jumuiya ya kimataifa kushindwa kutatua tatizo ambalo linatuathiri sote.'
Katika miezi ya hivi karibuni, Pedro Sanchez amekuwa akiunga mkono suala la kutambuliwa rasmi taifa la Palestina na kusisitiza juu ya kusimamishwa mashambulizi ya jeshi la Israel katika ukanda huo.
Katika kikao chake na rais wa utawala wa Kizayuni, Waziri Mkuu wa Uhispania pia amekosoa siasa za utawala ghasibu wa Israel kuhusiana na mauaji ya kimabari huko Ghaza na kuutaka uzingatie na kutoa umuhimu kwa sheria za kimataifa.
Serikali ya Chile pia ilitangaza Jumanne iliyopita kwamba itaondoa majina ya makampuni ya Israel kwenye orodha ya washiriki wa maonyesho makubwa ya anga ya Kusini mwa Marekani yatakayofanyika Santiago.
342/