Gazeti hilo limeandika kuwa vyanzo vya Marekani vilitangaza kwa vyombo vya habari vya kimataifa kwamba juhudi za nchi hiyo za kukomesha mashambulizi ya wapiganaji wa Yemen dhidi ya meli zinazoelekea Isarel kwenye Bahari ya Shamu zinatatizwa na ukosefu wa taarifa za kijasusi kuhusu silaha za Ansarullah na uwezo wao kamili wa kijeshi.
Gazeti la Izvestia limeongeza kuwa, Pentagon haijui athari za uharibifu iliowasababishia wapiganaji wa Kihouthi kupitia mashambulizi yaliyofanyika nchini Yemen, kwani hapo awali haikuwa na taarifa za kina kuhusu ukubwa wa silaha na zana za kivita za wapiganaji hao wa Yemen.
Limeongeza kuwa, inawezekana kwamba harakati ya Ansarullah inaficha silaha zake kwa uangalifu mkubwa kwa kutumia maficho ya chini ya ardhi katika maeneo ya milimani, sambamba na nia ya kundi hilo ya kuchukua hatua zote za dharura za kulinda taarifa za ndani dhidi ya uvujaji.Ripoti hiyo imemnukuu Ted Singer, afisa mkuu wa zamani wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), akisema kuwa kupata taarifa za ujasusi kuhusu Yemen imekuwa kazi ngumu tangu Washington ilipoondoa ubalozi wake katika mji mkuu wa Yemen, Sanaa, mwaka 2015, baada ya wapiganaji wa Ansarullah kuudhibiti mji huo. Katika upande mwingine, kiongozi wa harakati ya Ansarullah amesisitiza uungaji mkono usio na kikomo wa taifa la Yemen kwa kadhia ya Palestina na kusema kuwa, vikosi vya jeshi la nchi hiyo vitaendeleza mashambulizi ya kulipiza kisasi katika Bahari Nyekundu dhidi ya meli za Marekani, Israel Uingereza na washirika wao katika mwezi mtukufu wa Ramadhani. Sambamba na kushadidi mashambulizi ya utawala wa Kizayuni wa Israel katika Ukanda wa Ghaza, wanajeshi wa Yemen wameamua kuzuia meli zote zinazohusiana na utawala huo katili na zile zilizoko safarini kuelekea Israel. Operesheni hizo zimewasababishia hasara kubwa Wazayuni na ndio maana madola ya kibeberu ya Marekani na Uingereza yameanzisha vita dhidi ya Yemen ili kuunga mkono jinai za Israel huko Gaza.