Main Title

source : Parstoday
Jumapili

17 Machi 2024

20:13:43
1445195

Waziri wa Ulinzi: Iran iko tayari kuisaidia Syria kuimarisha nguvu zake za kiulinzi na za kuzuia mashambulio

Waziri wa Ulinzi wa Iran Brigedia Jenerali Mohammad Reza Ashtiani amesema Jamhuri ya Kiislamu iko tayari kutumia uwezo wake wote kuisaidia Syria katika kuimarisha ulinzi na uwezo wake wa kuzuia hujuma za Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Katika mkutano aliofanya na mwenzake wa Syria Ali Mahmoud Abbas mjini Tehran jana Jumamosi, Ashtiani alionya dhidi ya njama za Marekani na Israel za kuzidisha mgogoro katika eneo la Asia Magharibi. Amesema, kosa lolote la kistratijia na chokochoko za Marekani na utawala wa Kizayuni zitapelekea hali kuwa mbaya zaidi katika eneo hili. Brigedia Jenerali Ashtiani amelaani mashambulizi ya anga yanayofanywa na Israel dhidi ya Syria na ukiukaji wa mamlaka ya ardhi ya nchi hiyo na akasema, utawala huo ghasibu unalenga kuharibu miundombinu ya nchi hiyo kama vile viwanja vya ndege na bandari na kushambulia misafara ya kubeba mafuta na chakula kwa kisingizio cha mapambano dhidi ya Muqawama. Waziri wa Ulinzi wa Iran amesema ana imani kuwa mashambulizi ya Israel yanatokana na hofu na kushindwa utawala huo ghasibu.Amesisitiza umuhimu wa kuimarishwa uwezo wa kuzuia hujuma ili kukabiliana na mashambulizi ya Israel na kubainisha kuwa, hatua na mipango ya lazima na ya dharura iko katika ajenda zitakazofanyiwa kazi na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ili kukabiliana na uchokozi wa utawala huo ghasibu.

 Ashtiani amebainisha kuwa uwepo "haramu na ukaliaji ardhi kinyume cha sheria na usio na uhalali" wa Marekani nchini Syria ni ukiukaji wa wazi wa kanuni za kimsingi za sheria za kimataifa na Mkataba wa Umoja wa Mataifa. Ameashiria pia hali nyeti na ngumu katika eneo akisema, zaidi ya Wapalestina 31,000 wameuawa shahidi na zaidi ya 70,000 wamejeruhiwa wakati wa vita vya mauaji ya kimbari ya Israel dhidi ya Ghaza katika kipindi cha miezi mitano iliyopita. Waziri wa Ulinzi wa Iran amekosoa pia Umoja wa Mataifa na Baraza la Usalama la umoja huo kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao wa kimataifa kuhusiana na jinai za kivita za Israel na mauaji ya kimbari unayofanya huko Ghaza na kusisitiza kwamba utawala huo ghasibu bila shaka utashindwa kufikia lolote kati ya malengo yake katika Ukanda huo. Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi wa Syria amesema, matukio ya Ghaza na mauaji ya watu wasio na hatia wa Palestina yamefichua nguvu duni na dhaifu za Israel na kufichua tabia ya unafiki na uzandiki ya Marekani na Magharibi.

Abbas ameongeza kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel unaoua watoto umezidisha hali ya wasiwasi katika eneo hususan katika nchi za Syria na Lebanon baada ya kushindwa kufikia malengo yake huko Ghaza na kutumia uungaji mkono wa Muqawama na Iran kwa wananchi madhulumu wa Palestina kama kisingizio cha kuziandama nchi hizo.

Waziri wa Ulinzi wa Syria amebainisha kuwa, kuwepo kinyume cha sheria Marekani nchini Syria kumeifanya nchi hiyo kuwa kituo cha uungaji mkono kwa makundi yanayotaka kujitenga na ya kigaidi.

Aidha amekumbusha kuwa, Muqawama na kuimarishwa ushirikiano wa kiulinzi kati ya Tehran na Damascus ndio njia bora za kukabiliana na maadui.../