Wizara ya Afya ya Palestina imeeleza kuwa katika muda wa saa 24 zilizopita wanajeshi vamizi wa utawala wa Kizayuni umewauwa shahidi watu 72 na kuwajeruhi 114 baada ya kutekeleza visa saba vya mauaji kwa familia za Ukanda wa Gaza jana Jumamosi.
Watu wengi bado wapo chini ya vifusi na barabarani kwa kuwa wafanyakazi wa huduma za uokoaji wameshindwa kufika katika maeneo hayo.
Utawala haramu wa Israel umeendelea kupuuza uamuzi wa muda wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ) na unaendelea kutekeleza mauaji ya kimbari dhidi ya wakazi waso na ulinzi wa Ukanda wa Gaza. Hadi sasa Wapalestina wasiopungua 32,142 wameuawa shahidi , wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na wengine 74,412 kujeruhiwa tangu Oktoba 7 mwaka jana.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa imeeleza kuwa vita vya Israel dhidi ya Gaza vimesababisha asilimia 85 ya wakazi wa eneo hilo kuwa wakimbizi wa ndani huku kukiwa na uhaba mkubwa wa chakula, maji safi na dawa. Aidha asilimia 60 ya miundombinu ya eneo hilo imeharibiwa au haifanyi kazi.
342/