Shirikisho la Soka la Palestina hivi karibuni lilituma rasmi barua kwa FIFA liikitaka taasisi hiyo ya kimataifa ya kandanda duniani kuliwekea vikwazo Shirikisho la Soka la utawala wa Israel kufuatia vitendo vya ukiukaji vinavyofanywa na wanajeshi vamizi wa Israel kwa sekta ya michezo ya Palestina.
Katika taarifa yake hiyo, Shirikisho la Mpira wa Miguu la Palestina limetaka suala la kuuwekea vikwazo utawala wa Kizayuni liwekwe katika ajenda ya kazi ijayo ya mkutano wa FIFA utakaofanyika Machi 17 mwaka huu huko Thailand.
Mehdi Taj, Rais wa Shirikisho la Soka la Iran katika barua yake kwa Katibu Mkuu wa FIFA ametangaza kuwa anaunga mkono kikamilifu kujumuishwa katika ajenda ya Kongamano la 74 la FIFA huko Bangkok pendekezo la Shirikisho la Soka la Palestina kuhusu kuliwekea vikwazo Shirikisho la Soka la utawala wa Kizayuni. Barua ya Mkuu wa Shirikisho la Soka la Iran imeeleza kuwa: "Mpango huu wa Shirikisho la Soka la Palestina unahusu kudhihirisha suala la umoja, mshikamano na utu, masuala ambayo yote ni misingi ya moyo wa soka; aidha tunafurahia kujitolea kwao katika kuendeleza amani na umoja kupitia michezo, hasa katika mazingira haya magumu yanayowakabili."
342/