Kamandi Kuu ya Jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetoa tamko hilo katika taarifa yake ya Jumamosi kwa mnasaba wa mwaka wa 45 wa kuasisiwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Taarifa hiyo Imesema siku hiyo ni moja ya wakati muhimu zaidi katika historia ya Iran ambapo taifa la Iran liliweza kudhihirisha azma ya kuamua hatima yake na kupinga utawala wa madola ya kigeni nchini.
Taarifa hiyo imesema Mfumo wa Kiislamu wenye nguvu na wa kidemokrasia umeweka mkazo wake juu ya uhuru wa kisiasa na kujitegemea na sasa Iran imegeuka kuwa kielelezo kwa mataifa yote yanayotafuta uhuru wa kweli duniani kote.
Aidha Jeshi la Iran limesisitiza kuwa, licha ya njama zinazoendelea za maadui, lakini fikra na siasa za Jamhuri ya Kiislamu ziko nje ya mipaka ya kijiografia kwa kuzingatia sera za nchi hii za kupinga dhulma na ubeberu na kuanzisha mfumo wa demokrasia ya kidini na uungaji mkono wake kwa watu wanaodhulumiwa kote duniani.
Hali kadhalika taarifa hiyo imesema Jamhuri ya Kiislamu imeongeza matumaini ya mataifa yote yanayotaka kusambaratisha ubeberu wa madola ya Magharibi hususan Marekani, Uingereza na nchi zingine kadhaa za Ulaya.
Katika kura ya maoni ya siku mbili ya kihistoria iliyofanyika Machi 30-31, 1979, takriban asilimia 98.2 ya Wairani waliostahiki walipiga kura ya "ndio" kwa ajili ya kuanzishwa Jamhuri ya Kiislamu hapa nchini.
Kura hiyo iliyopigwa chini ya miezi miwili baada ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu inachukuliwa kuwa hatua ya kuleta mabadiliko katika historia ya kisasa ya Iran.
342/