Kwa mujibu wa shirika la habari la FARS, Rais Ebrahim Raisi amesema hayo usiku wa kuamkia leo Jumatatu katika mkesha wa Laylatul Qadr na kusisitiza kuwa, leo hii mizozo iliyopo baina ya Waislamu inatumiwa vibaya na utawala wa Kizayuni.
Vilevile amesema Laylatul Qadr ni usiku wenye hadhi na cheo kikubwa na ni wajibu kwa Waislamu kuuhuisha usiku huo uliojaa nuru, kwa kufanya ibada nyingi ndani yake.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, Waislamu wanapaswa kuelewa kwamba njia ya wokovu wao wa duniani na Akhera ni kushikamana na hoja za Mwenyezi Mungu na mafundisho yake matakatifu yaliyomo kwenye Qur'ani Tukufu.
Amezungumzia pia Siku ya Kimataifa ya Quds ambayo ni Ijumaa ya mwisho ya mwezi mtukufu wa Ramadhani na ambayo kwa mwaka huu imeangukia kwenye Ijumaa ya wiki na kuongeza kuwa, wanaopaza sauti zao katika Siku ya Kimataifa ya Quds wanatekeleza nasaha zilezile za Imam Ali AS alizompa mwanawe Imam Hasan AS kabla ya kuuawa shahidi baada ya kupigwa upanga wenye sumu akiwa kwenye Sijda na kusababisha kifo chake.
Kabla ya hapo pia, Rais Ebrahim Raisi alikuwa amesema kwamba Qur'ani Tukufu imetilia mkazo mno wajibu wa kuweko umoja na mshikamano madhubuti baina ya Waislamu na siri ya kufanikiwa umma huu ni kushikamana vilivyo na mafundisho yaliyomo kwenye aya za Kitabu hicho Kitakatifu.
342/