Main Title

source : Parstoday
Jumatatu

1 Aprili 2024

14:18:06
1448210

Iran na Misri zataka kufanyike juhudi madhubuti za kuizuia Israel isiuvamie mji wa Rafah

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Iran na Misri wametoa mwito wa kuchukuliwa hatua za maana kimataifa ili kuzuia mashambulizi ya kivamizi ya utawala wa Kizayuni katika mji wa Rafah wa kusini mwa Ukanda wa Ghaza.

Hossein Amir-Abdollahian, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amefanya mazungumzo ya simu na Sameh Hassan Shoukry, waziri mwenzake wa mambo ya nje wa Misri na kujadiliana naye njia za kuhakikisha utawala wa Kizayuni hauuvamii mji wa Rafah ambao sehemu kubwa ya wananchi wa Ghaza wamekimbilia huko.

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Iran na Misri wamepinga njama zote za utawala wa Kizayuni za kutaka kuwahamisha kwa nguvu Wapalestina kwenye Ukanda wa Ghaza  na kuhimiza kuchukuliwa hatua za kimataifa za kuzuia jinai zaidi za Israel huko kusini mwa Ghaza. 

Mawaziri hao wameelezea pia kuridhishwa kwao na juhudi zilizofanywa na pande hizi mbili katika miezi ya hivi karibuni kwa ajili ya kuimarisha uhusiano baina yao na kuelezea matumaini yao kuwa viongozi wa kisiasa wa nchi hizi mbili za Kiislamu watachukua hatua kubwa zaidi ya kurejesha uhusiano baina ya Tehran na Cairo ambao kwa hakika ni muhimu kwa ulimwengu mzima wa Kiislamu na kwa utulivu na amani ya eneo hili zima.

342/