Kwa mujibu wa shirika la habari la Mehr, leo Jumanne na katika siku ya 179 ya uvamizi na mashambulio dhidi ya Ukanda wa Ghaza, ndege za kivita za Israel zimeshambulia maeneo ya makazi ya watu magharibi mwa mji wa Rafah, ambapo idadi kadhaa ya raia wa Palestina wameuawa shahidi au kujeruhiwa.Msikiti wa Al-Bashir ulioko Deir al-Balah umeshambuliwa pia na ndege za kivita za utawala wa Kizayuni, ambapo kwa uchache mtoto mmoja wa Kipalestina ameuawa shahidi na watu 20 wamejeruhiwa.
Ripoti nyingine kutoka Ghaza zinasema, katika jinai ya hivi karibuni, jeshi la utawala wa Kizayuni limeshambulia wafanyakazi wa kigeni wa utoaji misaada huko Deir al-Balah, katikati ya Ukanda wa Ghaza.
Katika shambulio hilo, jeshi la Israel limelenga gari la shirika la kimataifa la usambazaji misaada ya kibinadamu, na kuua watu saba raia wa kigeni waliokuwemo ndani ya gari hilo.Ofisi ya Habari ya Serikali ya Palestina katika Ukanda wa Ghaza imelaani jinai hiyo mpya ya utawala wa Kizayuni ya kushambulia wafanyakazi wa kimataifa wa utoaji misaada na kuzitaka taasisi za kimataifa zilaani vitendo vya kinyama vya utawala huo ghasibu. Habari nyingine kutoka Palestina inayokaliwa kwa mabavu zinasema, wanajeshi wa Kizayuni wameshambulia kambi ya Qalandiya iliyoko kaskazini mashariki mwa Quds inayokaliwa kwa mabavu katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan leo asubuhi.
Shirika la Hilali Nyekundu la Palestina limetangaza pia kuwa, Wapalestina wasiopungua wawili wamejeruhiwa katika shambulio la wanajeshi wa Kizayuni kwenye kambi ya Qalandiya. Wanajeshi hao wa Kizayuni wameshambulia pia kijiji cha Dairul-Bari magharibi mwa Ramallah, kitongoji cha Katiful-Wad katika mji wa Ariha, eneo la Sanjal kaskazini mwa Ramallah, mji wa Dora ulioko kusini mwa Al-Khalil na eneo la Urif kusini mwa Nablus na kuwatia nguvuni Wapalestina kadhaa.../