Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa JMAT, Sheikh Dkt. Alhad Mussa Salum, amesema matamshi na vitendo vya namna hiyo si vya kiungwana na vinatishia mshikamano na maelewano baina ya nchi jirani na marafiki.
Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Dar es Salaam – Mei 29, 2025 - Viongozi wa dini kupitia Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT) wameeleza masikitiko yao makubwa kufuatia vitendo vya baadhi ya vijana wa Kenya kumkosea heshima Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa JMAT, Sheikh Dkt. Alhad Mussa Salum, amesema matamshi na vitendo vya namna hiyo si vya kiungwana na vinatishia mshikamano na maelewano baina ya nchi jirani na marafiki.
"Tulipofika panatosha. Moto mkubwa huanza na moto mdogo. Hatuwezi kukaa kimya tukiona viongozi wetu wanakosewa heshima bila sababu za msingi," alisema Sheikh Dkt. Alhad kwa msisitizo.
Katika hotuba yake, Sheikh Dkt.Alhad amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuwasamehe vijana waliotenda kosa hilo, akisema kuwa vijana hao walikosea lakini bado wana nafasi ya kujifunza na kurekebisha mienendo yao.
"Tunamuomba Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan asamehe vijana wa Kenya waliomkosea heshima. Tunaamini hawakuelewa uzito wa walichokifanya." alisema Sheikh Dkt. Alhad Mussa Salum, ambaye ni Mwenyekiti wa JMAT-TAIFA.
Kwa ujumla, Viongozi wa JMAT pia wamewataka vijana wa Afrika Mashariki kuheshimu viongozi na kuhakikisha kuwa tofauti za kisiasa au kijamii hazileti chuki, kejeli au kuvunjiana heshima.
Tumekuwekea hapa chini baadhi ya picha za mkutano huo wa Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania, ukiongozwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT-TAIFA), Sheikh Dkt. Alhad Mussa Salum, na Katibu Mkuu wa JMAT-TAIFA, Askofu Dkt. Gabriel Ole Maasa.
Your Comment