Kikao hiki kimeacha athari chanya kwa walimu na wahudumu, na kimeimarisha dhamira ya pamoja ya kuhakikisha kuwa Jamiat Al-Mustafa (s) inaendelea kutoa mchango wake katika kuelimisha, kulea na kuinua jamii kitaaluma, kimaadili na kiutamaduni.
Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) - ABNA- Dar es Salaam, 27 Agosti 2025 – Rais wa Jamiat Al-Mustafa (s) tawi la Dar es Salaam, Tanzania, Dr. Ali Taqavi, ameongoza kikao kazi maalum na walimu pamoja na wahudumu wa Chuo cha Kisayansi cha Jamiat Al-Mustafa (s) kilichopo Mbezi Beach, Dar es Salaam.
Malengo ya Kikao
Katika kikao hicho, Dkt. Ali Taqavi alisisitiza juu ya umuhimu wa kuendeleza juhudi kubwa katika kuboresha na kuimarisha idara mbalimbali za chuo, zikiwemo:
- Idara ya Taaluma.
- Idara ya Utafiti.
- Idara ya Masuala ya Ndani na Ofisi.
- Idara ya Utamaduni.
- Idara ya Mahusiano ya Umma na Kimataifa.
Aidha, alisisitiza kuwa juhudi hizi zinalenga kuhakikisha kuwa chuo kinabaki kuwa kitovu cha maarifa, malezi ya kimaadili na daraja la uhusiano mwema wa kimataifa.
Wito wa Kujituma na Uchapaji Kazi
Hujjatul Islam wal-Muslimin, Dkt. Ali Taqavi aliwakumbusha walimu na wahudumu wote juu ya wajibu wa kujituma katika kazi na kuhakikisha kila jukumu linafanywa kwa kiwango cha juu na ubora wa hali ya juu. Alisema kuwa ubora wa kazi ndiyo msingi wa matokeo bora ambayo huchangia maendeleo ya jamii ya Mwanadamu, na akaashiria katika muktadha huo juu ya kauli ya Mwenyezi Mungu (swt) aliposema katika Qur’an Tukufu:
“Na sema: Fanyeni kazi, basi Mwenyezi Mungu atayaona matendo yenu, na Mtume wake, na Waumini.”
(Surat At-Tawbah, 9:105).
Aya hii inatoa msisitizo kwamba kila juhudi ya mja haina budi kufanywa kwa nia safi na kwa kiwango cha juu, kwani matendo hayo yanaangaliwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake (saww) na Waumini.
Mchango wa Fikra wa Walimu na Wahudumu
Katika kikao hiki, walimu wote walipata nafasi ya kuwasilisha mawazo na mapendekezo yao juu ya njia bora za kuinua kiwango cha kazi na kuongeza ufanisi. Hoja zao ziliweka msukumo mpya wa fikra na ubunifu kwa mustakabali wa chuo.
Katika Hadithi Maarufu, Mtume Muhammad (s.a.w.w) amesema:
“Hakika Mwenyezi Mungu anapenda mtu anapofanya kazi, aifanye kwa ubora zaidi.”
Hadithi hii inasisitiza kwamba kufanya kazi kwa weledi, kujituma na kwa moyo wa ihsan ni sehemu ya ibada na ni njia ya kuleta maendeleo ya kweli katika jamii.
Kwa Ujumla:
Kikao hiki kimeacha athari chanya kwa walimu na wahudumu, na kimeimarisha dhamira ya pamoja ya kuhakikisha kuwa Jamiat Al-Mustafa (s) inaendelea kutoa mchango wake katika kuelimisha, kulea na kuinua jamii kitaaluma, kimaadili na kiutamaduni.
Mwenyezi Mungu Azibariki Juhudi Hizi.
Your Comment