26 Oktoba 2020 - 12:18
Jibu la Msemaji wa Baraza la Kulinda Katiba kwa madai ya Washington

Ikulu ya rais wa Marekani, White House imeituhumu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuwa inaingilia uchaguzi wa rais wa nchi hiyo. Madai hayo yametolewa kwa kutegemea baadhi ya baruapepe zilizodaiwa zimetumwa na baadhi ya wadukuzi wa Kiirani kwa raia wa Marekani kwa shabaha ya kuvuruga au kuathiri matokeo ya uchaguzi wa nchi hiyo.

Shirika la habari la Ahlubayt (as)ABNA: Baada ya madai hayo, Marekani imeziwekea vikwazo baadhi ya taasisi za vyombo vya habari za Iran. Makelele haya ya kipropaganda kuhusu madai ya Iran kuingilia uchaguzi wa rais wa Marekani na kuwekewa vikwazo taasisi za vyombo vya habari za Iran yanaweza kuwa ni hatua ya makusudi ya kutaka kupotosha au kuficha fedheha zinazoandamana na uchaguzi wa Marekani na fazaa ya kisiasa inayotawala nchi hiyo katika kipindi cha sasa. 

Msemaji wa Baraza la Kulinda Katiba la Iran, Abbas Ali Kadkhodaei amejibu madai hayo ya Marekani na kusema: Iran imekuwa ikitangaza kuwa, haiingilii masuala ya ndani ya nchi nyingine, na zaidi ni kwamba haina haja ya kufanya hivyo. Kadkhodaei ameongeza kuwa: Donald Trump anapaswa kuelewa kuwa zama za nchi moja kuingilia masuala ya ndani ya nchi nyingine zimeyoyoma na kutoweka. 

Kwa ujumla suala hilo tunaweza kulichunguza kwa mitazamo tofauti. Kwanza ni kwamba, kwa miaka mingi sasa Marekani imekuwa ikiingilia masuala ya ndani ya nchi nyingine duniani ikiwemo Iran kwa kutumia kisingizio cha kuimarisha au kusimika demokrasia na au kurejesha amani katika nchi hizo.  

Pili ni kwamba, nyaraka na ushahidi mwingi unaonyesha kuwa, wachezaji wa kigeni wenye taathira katika maamuzi na mwenendo wa kisiasa wa Marekani ni lobi za Wasaudia na utawala wa Kizayuni wa Israel katika fremu ya jumuiya ya AIPAC. 

Taasisi ya RAN POL imeandika katika ripoti yake kuhusu madai hayo kwamba, madai ya kutumwa baruapepe 1500 kutoka Iran, hata kama yatakuwa ya kweli, hayawezi kuwa na taathira katika uchaguzi wa rais wa Marekani; na hata madai kuwa Russia inaingilia uchaguzi huo pia yanaonekana kuwa ni mbinu ya kipropaganda na wala si tishio la usalama.

Gazeti la New York Times pia limeandika uchambuzi kuhusu madai hayo na kusema: Kuna uwezekano Donald Trump mwenyewe ndiye aliyeanzisha mchezo huo. Kwa wiki kadhaa sasa Trump amekuwa akidai kuwa kutafanyika udanganyifu katika uchaguzi wa rais bila ya kutoa ushahidi wa aina yoyote. Anadai kufanyika uchaguzi kupitia njia ya posta kutasababisha udanganyifu na kwamba njia pekee itakayowawezesha washindani wake kumshinda ni kufanya udanganyifu.…

Inaonekana kweli kwamba madai kuwa nchi za kigeni zinaingilia zoezi la uchaguzi wa Marekani ni mbinu ya kipropaganda inayofanyika kupitia njia ya kusambaza ripoti na habari zisizo zahihi na bandia.

Mchambuzi wa masuala ya kisiasa ya kimataifa Ali Beigi amezungumzia sababu na chanzo cha madai haya yanayotolewa na maafisa wa serikali ya Marekani na kusema: "Madai kuwa Iran inaingilia uchaguzi wa rais wa Marekani ni mbinu inayolenga kutengeneza hali ya kudhulumiwa na kuonewa Donald; na hata masuala kama kulazwa hospitalini kiongozi huyo kwa madai ya virusi vya corona, yote hayo yamefanyika kwa lengo hilo."

Alaa kulli hal, kama alivyosisitiza msemaji wa Baraza la Kulinda Katiba la Iran, uchaguzi wa Marekani ni suala la ndani ambalo Iran haina hamu wala haioni ulazima wa kuingilia.    

342/