18 Septemba 2024 - 19:19
Araghchi: Kuunga mkono muqawama dhidi ya Israel ni 'sera ya kimsingi' ya Iran

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Sayyid Abbas Araghchi amesisitiza kuhusu sera thabiti ya Jamhuri ya Kiislamu ya kuunga mkono vikosi vya muqawama katika mapambano yao dhidi ya utawala ghasibu wa Israel.

Araghchi a,etoa ahadi hiyo wakati wa mkutano na Salah Fahs, mwakilishi wa Harakati ya Amal ya Lebanon mjini Tehran.

Katika kikao hicho, Fahs amewasilisha pongezi za spika wa bunge la Lebanon na mwenyekiti wa Harakati ya Amal, Nabih Berri, kwa Araghchi kwa kuteuliwa kuwa waziri wa mambo ya nje wa Iran.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amepongeza hatua za Berri za kuunga mkono mapambano na pia kujitolea mhanga wapiganaji wa Harakati yake ya Amal pamoja na wanachama wa Hizbullah katika vita dhidi ya hujuma za Israel dhidi ya Lebanon na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi ya juu wa Iran pia amesisitiza kuhusu sera ya kimsingi ya Iran ya kuunga mkono vikosi vya muqawama katika mapambano yao halali dhidi ya utawala wa Kizayuni.

Araghchi na Fahs pia wamejadili matukio  ya hivi karibuni ya kikanda, ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya Israel nchini Lebanon, hali ya mambo katika maeneo ya Wapalestina na vita vinavyoendelea vya Israel vya mauaji ya kimbari dhidi ya Gaza.

342/