Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) - ABNA - Kwa mujibu wa gazeti la Al-Quds Al-Arabi, matokeo ya uchaguzi wa hivi karibuni nchini Kanada yamezua hasira kubwa katika duru za wafuasi wa utawala wa Kizayuni. Hali hii imejitokeza hasa kutokana na ushindi wa chama cha Liberal kinachoongozwa na Mark Carney, ambaye katika suala la Palestina, anachukuliwa kuwa na mtazamo wa tahadhari zaidi kuliko wa chuki ya wazi, ingawa hana mpango wa kufanya mabadiliko ya msingi.
Aviva Klompas, aliyekuwa mwandishi wa hotuba za ujumbe wa Israel katika Umoja wa Mataifa na mzaliwa wa Toronto, ameonesha hali ya kukata tamaa kubwa kutokana na matokeo hayo. Vilevile, Dalia Kurtz, mshawishi (influencer) maarufu wa Kizayuni, ametangaza nia ya kuhamia Florida, akidai kuwa Kanada imekuwa kama “Jamhuri ya Kiislamu ya Kanada.”
Kauli hizi za wafuasi wa Israel zinaonyesha hofu yao kuhusu kupungua kwa uungaji mkono wa wazi kwa utawala wa Kizayuni, hasa ikizingatiwa kuwa Mark Carney hana mwelekeo wa kiitikadi wa wazi kama mtangulizi wake, Justin Trudeau, ambaye katika siku za mwisho za uongozi wake alijitangaza waziwazi kuwa “Mzayuni.”
Ingawa Carney hakuchukua msimamo wa moja kwa moja dhidi ya ukatili wa Israel, alipohojiwa kuhusu mauaji ya Wapalestina alisema hilo ni “swali gumu” na hakutoa jibu la moja kwa moja. Wakati wa kampeni, alipoambiwa na mmoja wa waliokuwepo kuwa “kuna mauaji ya halaiki yanayoendelea Palestina,” alijibu kwa kusema:
“Ninalifahamu hilo, na ndiyo maana tumetangaza marufuku ya uuzaji wa silaha kwa Israel.”
Hata hivyo, baadaye alijaribu kujiondoa kwenye kauli hiyo, akisema:
“Sikusikia mtu akitumia neno ‘mauaji ya halaiki’.”
Kauli hizi zinaonesha njia ya tahadhari anayochukua Carney katika kuendesha siasa za nje, jambo ambalo linawatia wasiwasi wale waliokuwa wakitegemea sera za wazi za kuunga mkono Israel bila masharti.
Your Comment