Zaidi ya watu 50 wamekufa nchini Colombia, baada ya maporomoko ya ardhi kulikumba eneo la kaskazini magharibi mwa nchi hiyo jana.
Maafa hayo yamesababishwa na mvua kubwa iliyonyesha katika eneo hilo.
Wimbi la matope na taka taka viliukumba mji wa Salgar muda mfupi kabla ya alfajiri. Maafisa wanasema hawawezi kuthibitisha ni watu wangapi bado hawajulikani walipo.
Rais wa Colombia Juan Manuel Santos anasema kuwa utawala wa nchi hiyo haujui ni watu wangapi ambao hawajulikani waliko kufuatia maparomoko makubwa ya ardhi ambayo yamewaua zaidi ya watu 50.
Waakazi wa mji wa magharibi wa Salgar wanasema kuwa nyumba wanakoishi watu maskini zilisombwa na matope pamoja na mawe kufuatia mvua kubwa iliyonyesha eneo hilo.
Makundi ya uokoaji yanatafuta kwenye vifusi kujaribu iwapo yatapata manusura.
Rais ameitaja hali hiyo kuwa janga la kitaifa na kusema kuwa atazijenga upya nyumba zilizoaharibiwa.