8 Machi 2025 - 17:44
Source: Parstoday
"Kutokomeza umaskini miongoni mwa wanawake kutachukua miaka 130"

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres ameashiria matatizo yanayoendelea kuwakabili wanawake na wasichana duniani kote, akionya kwamba "kutokomeza umaskini uliokithiri miongoni mwa wanawake na wasichana kutachukua miaka 130."

Guterres alisema hayo jana Ijumaa katika hafla iliyofanyika kwa mnasaba wa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake huko New York na kuongeza kuwa, "Kila baada ya dakika 10, mwanamke mmoja anauawa na mpenzi wake au jamaa yake.

Ameeleza bayana kuwa, "Wanawake na wasichana zaidi ya milioni 612 wanaishi katika kivuli cha migogoro ya silaha - ambapo haki zao mara nyingi hazizingatiwi." 

Akiashiria changamoto sugu ambazo zinalemaza maendeleo na ustawi, Guterres amesema: Kwa mwenendo huu, kutokomeza umaskini uliokithiri kwa wanawake na wasichana kunaweza kuchukua miaka 130.

"Wanawake bado wanakabiliwa na vikwazo vya kimfumo - ghasia, ubaguzi, na ukosefu wa usawa wa kiuchumi - ambao umejikita sana katika jamii zetu," amesisitiza Katibu Mkuu wa UN.

"Kutokomeza umaskini miongoni mwa wanawake kutachukua miaka 130"

Guterres pia amekiri juu ya hatua na mafanikio yaliyopatikana tangu Azimio la Beijing la 1995, ambalo lilithibitisha tena kwamba "haki za wanawake ni haki za binadamu."

Amesema wasichana wengi hivi sasa wako shuleni, na wanawake wengi zaidi wanashikilia nyadhifa za madaraka, lakini anasisitiza kuwa mafanikio haya yanasalia kuwa tete.

342/

Your Comment

You are replying to: .
captcha