3 Mei 2025 - 23:21
Source: ABNA
Israel yafanya mashambulio 20 dhidi ya Syria, makali zaidi kushuhudiwa tangu ulipoanza mwaka 2025

Duru za habari zimeripoti kuwa, usiku wa kuamkia leo, utawala wa Kizayuni wa Israel umefanya mashambulio yasiyopungua 20 ya anga dhidi ya viunga vya mji  mkuu wa Syria Damascus, Dara’a, na Hama yakiwa ndio makali zaidi dhidi ya nchi hiyo tangu ulipoanza mwaka huu wa 2025.

Kwa mujibu wa duru hizo, mashambulizi hayo yamejumuisha kambi ya zamani ya jeshi la Syria karibu na kijiji cha Shatha huko Hama, makao makuu ya kikosi cha jeshi la zamani la Syria kaskazini mwa Damascus, na kambi za kijeshi huko Dara'a.

Miripuko imeripotiwa Damascus na kwenye vitongoji vyake, ikiwa ni pamoja na Harasta, ambapo maafa ya raia yamethibitishwa.

Vyombo vya habari vya utawala wa Kizayuni vimesema baadhi ya maeneo ya mji mkuu Damascus yamelengwa kwa mara ya kwanza.

Tangu serikali ya Rais Bashar Assad ilipoanguka mwezi Disemba, Syria imekuwa ikiandamwa na hujuma na mashambulio ya kijeshi ya utawala ghasibu wa Israel katika maeneo makubwa ya kusini mwa nchi hiyo.

Aidha, imekumbwa na mamia ya mashambulizi ya anga ya utawala huo wa Kizayuni ambayo yamekuwa yakilenga zaidi miundo mbinu ya kijeshi iliyokuwa ya jeshi la zamani la Syria.

Mapema siku ya Ijumaa, ndege za kivita za utawala ghasibu wa Israel zilishambulia karibu na ikulu ya rais wa Syria mjini Damascus, likiwa ni shambulio la pili la utawala huo haramu dhidi ya nchi hiyo ya Kiarabu wiki hii huku kukiwa na ukimya wa utawala unaoongozwa na Hay'at Tahrir al-Sham (HTS).

Operesheni za kijeshi za Israel nchini Syria zinafanyika katika hali ambayo waziri wa vita wa utawala huo wa Kizayuni Israel Katz alitangaza siku ya Jumapili kuwa Israel inapanga kuweka vikosi vyake vamizi kusini mwa Lebanon na Syria "kwa muda usiojulikana".../

342/

Your Comment

You are replying to: .
captcha