Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA- Rais wa Venezuela, Nicolás Maduro, ambaye katika siku za karibuni aliripotiwa kutekwa nyara kufuatia uvamizi wa Marekani mjini Caracas na kisha kuhamishwa kwa nguvu hadi New York, amefikishwa mahakamani pamoja na mkewe kwa tuhuma za ulanguzi wa dawa za kulevya.
Akizungumza mbele ya mahakama, Maduro alisisitiza waziwazi kuwa yeye ni Rais halali wa Venezuela na akajitambulisha kama mfungwa wa vita, akisisitiza kuwa hana hatia na hakubali tuhuma zote zilizowasilishwa dhidi yake. Alirudia msimamo huo huo hata alipokuwa akiondoka katika jengo la mahakama.
Kwa upande wake, mke wa Maduro pia alikana mashtaka ya ulanguzi wa dawa za kulevya yaliyofunguliwa dhidi yake nchini Marekani, akitangaza kuwa hana hatia.
Wakili wa Maduro ameliambia gazeti la New York Times kuwa kwa sasa hawajawasilisha ombi la kuachiwa kwa dhamana, ingawa uwezekano huo unaweza kuzingatiwa baadaye.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, Maduro alimwambia jaji kuwa kabla ya kufikishwa mahakamani, hakuwa ameona hati ya mashtaka wala hakuwa amepewa maelezo ya kutosha kuhusu haki zake za kisheria.
Mahakama ilimruhusu Maduro na mkewe kuwasiliana na ubalozi (konsula) wa nchi yao, huku wakili wake akibainisha kuwa mteja wake anataka kuachiliwa huru bila dhamana, lakini anaacha wazi haki ya kuomba dhamana siku zijazo.
Tukio hili limeibua mjadala mpana wa kimataifa kuhusu uhalali wa hatua za Marekani, athari zake za kisiasa, kisheria na kidiplomasia, pamoja na mustakabali wa uhusiano kati ya Washington na Caracas.
Your Comment