Kwa Mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) –ABNA–, timu ya taifa ya Iran inatarajiwa kuanza rasmi kampeni yake ya Kombe la Dunia 2026 kwa mchezo dhidi ya New Zealand katika Kundi G, baada ya kipindi kigumu cha miezi kadhaa kilichogubikwa na sintofahamu kuhusu ushiriki wake kutokana na hali ya usalama na mvutano wa kijeshi uliyoikumba nchi hiyo.
Mchezo huo utachezwa katika Uwanja wa Los Angeles, California, Marekani, huku ukionekana kuwa zaidi ya pambano la soka kwa Wairani wengi, bali pia ishara ya uthabiti na mshikamano wa taifa baada ya changamoto walizopitia.

Kocha wa Iran anatarajiwa kumtegemea mshambuliaji nyota, Mehdi Taremi, kuiongoza safu ya ushambuliaji dhidi ya New Zealand katika jitihada za kuanza mashindano hayo kwa ushindi muhimu.
Iran ipo Kundi G pamoja na New Zealand, Ubelgiji na Misri, ambapo kila pointi itakuwa muhimu katika mbio za kutinga hatua ya 16 bora. Mashabiki wa soka duniani wanasubiri kuona iwapo Iran itaweza kugeuza maandalizi yake magumu kuwa matokeo chanya uwanjani na kuanza safari yake ya Kombe la Dunia kwa mafanikio.

Your Comment