10 Septemba 2024 - 14:57
Jinai za Israel: Watoto 45,000 wa darasa la kwanza wameshindwa kuanza msimu mpya wa masomo Gaza

Wakati watoto wanajiandaa kwa ajili ya mwaka na siku yao ya kwanza shuleni katika nchi kadhaa za Mashariki ya Kati, takriban watoto 45,000 wenye umri wa miaka sita katika Ukanda wa Gaza wamenyimwa haki hii ya kuanza masomo kutokana na jinai za utawala haramu wa Israel.

Katika taarifa iliyotolewa mjini Amman Jordan siku ya Jumatatu, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) limesema wengi wao wamefurushwa kutoka katika makazi yao na kwamba wanapigana vita kila uchao ili kuweza kuishi.

Mwaka mpya wa masomo ulipaswa kuanza kote Palestina jana, lakini haujaanza katika Ukanda wa Gaza ambapo mashambulizi na mauaji ya kimbari yanayotekelezwa na utawala haramu wa Israel yanaendelea kuathiri vibaya wanafunzi, walimu na shule za ukanda huo.

Wanafunzi wa darasa la kwanza Gaza wanajiunga na watoto  wengine 625,000 ambao tayari wamenyimwa mwaka mzima wa masomo, na huku mzozo ukiendelea, wanakabiliwa na hatari kubwa ya kupitisha mwaka wa pili bila masomo.

Mkurugenzi wa UNICEF wa Asia Magharibi na Kanda ya Afrika Kaskazini Adele Khodr amesema "Watoto katika Ukanda wa Gaza wamepoteza makazi yao, wanafamilia, marafiki, usalama na utaratibu wa kawaida maishani. Pia wamepoteza hifadhi salama na msisimuko unaotolewa na shule na kuweka mustakabali wao bora katika hatari ya kuharibiwa na mzozo huu unaoendelea."

Matamshi hayo yanakuja wakati mashambulizi ya utawala haramu wa Israel dhidi ya Gaza tangu Oktoba mwaka jana yamepelekea Wapalestina wasiopungua 41,000 kuuawa shahidi, wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto.

342/