31 Mei 2024 - 14:30
Trump, Rais wa zamani wa Marekani apatikana na hatia ya makosa ya jinai

Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump amepatikana na hatia katika makossa 34 ya jinai katika kesi ya kihistoria ambayo huenda ikatikisa kampeni za uchaguzi wa rais mwaka huu wa 2024 nchini humo.

Trump, mwenye umri wa miaka 77  ni rais wa kwanza wa Marekani kuwahi kushtakiwa na kisha kupatikana na hatia ya makosa ya jinai.

Jopo la wajumbe wa mahakama moja jijini New York, Alhamisi lilimpata na hatia mtawala huyo wa  zamani wa Marekani kwa mashtaka 34 ya kugushi hati zake za biashara.

Hukumu ya Trump imepangwa kutolewa Julai 11, kati kati ya kampeni yake ya kutaka kuitawala tena Marekani, siku chache tu kabla ya kuanza kwa Kongamano la Kitaifa la chama chake cha Republican hapo Julai 15.

Rais huyo wa zamani, ambaye amekanusha mashtaka hayo dhidi yake, anatazamiwa kuchuana vikali na mgombea wa chama cha Democratic Joe Biden katika uchaguzi wa Novemba.

Trump anakabiliwa na kifungo cha hadi miaka minne jela kwa kila kosa, ingawa waangalizi wa mahakama wanasema kuna uwezekano kwamba atapunguziwa adhabu.

Akizungumza nje ya mahakama Trump amesema: "Hii ilikuwa kesi iliyoibwa na ya kufedhehesha. Hukumu ya kweli itakuwa ile ya wananchi mnamo Novemba 5. Wananchi wanajua kilichotokea hapa."


342/