Main Title

source : Parstoday
Jumamosi

3 Februari 2024

19:36:55
1434895

UN: Tishio la ugaidi ni kubwa katika maeneo yenye mizozo Afrika na Afghanistan

Tishio la ugaidi la mtandao wa kigaidi na kitakfiri wa al Qaida, kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) na makundi mengine yenye mfungamano na magenge hayo lingali kubwa katika maeneo yenye migogoro barani Afrika na huko Afghanistan, na viwango cha vitisho vinaongezeka katika baadhi ya maeneo ikiwemo barani Ulaya.

Haya yameelezwa na wataalamu wa Umoja wa Mataifa katika ripoti yao mpya. 

Jopo la wataalamu wa Umoja wa Mataifa limeeleza katika ripoti hiyo yenye kurasa 23 kwamba, bado kuna uhusiano wa karibu kati ya  watawala wa kundi la Taliban linaloongoza Afghanistan na mtandao wa al Qaida, na nchi kadhaa wanachama ambazo hazijatajwa majina, zimeeleza kuwa kuwepo kwa makundi ya kigaidi nchini humo kunadhoofisha hali ya usalama wa kikanda. 

Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wameongeza kuwa: Kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) lingali ni tishio kuu zaidi huko Afghanistan. Jopo hilo la UN limeeleza haya katika kikao cha Baraza la Usalama katika ripoti iliyoishia Disemba 13 mwaka jana. Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa awali waliashiria msururu wa mashambulizi ya kigaidi katika nchi jirani za Iran na Pakistan na vitisho vnavyozikabili nchi za Asia ya Kati. Inafaa kuashiria hapa kuwa, kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) lilijitenga na mtandao wa al-Qaida zaidi ya muongo mmoja uliopita na kisha likavuna wafuasi kutoka maeneo mbalimali dunia licha ya kushindwa huko Iraq mwaka 2017 na kisha huko Syria miaka miwili baadaye. Kundi hilo la Daesh lina wapiganaji kati ya 3,000 hadi 5,000 huko Syria na Iraq kwa pamoja. Kwa upande wa bara Ulaya, wataalamu wa Umoja wa Mataifa wamesema kuwa tisho rasmi la ugaidi limeongezeka barani humo. Mwaka 2023 mashambulizi hatari ya kigaidi yalitekelezwa huko Ufaransa na Ubelgiji pamoja na matukio mengi ya kigaidi yasiyo ya mauaji na kutiwa mbaroni kwa wanachama wa makundi hayo katika nchi kadhaa za Ulaya.

342/