29 Septemba 2024 - 18:17
Maafisa wa Marekani: Ni vigumu kwa Israel kuiangamiza Hizbullah

Gazeti la New York Times la Marekani limewanukuu maafisa wa serikali ya nchi hiyo wakisema kuwa, ni vigumu kwa Israel kufanikiwa kuharibu uwezo wa Hizbullah, huku kukiwa na tishio la jeshi la Israel la kuanzisha operesheni ya nchi kavu nchini Lebanon.

Maafisa hao wamesema kuwa Israel itapata ugumu wa kuiangamiza Hizbullah kama itafanya uvamizi wa nchi kavu katika ngome yake kusini mwa Lebanon.

Maafisa hao wa Marekani wamesisitiza kuwa, madhara kwa raia yatakuwa makubwa zaidi kuliko yale yaliyosababishwa na Israel katika Ukanda wa Gaza iwapo Netanyahu ataamua kushambulia safu ya kijeshi ya harakati hiyo.

Maafisa hao wa serikali ya Marekani wamedokeza kuwa Hizbullah itachukua hatua kali zaidi dhidi ya Israel kujibu mauaji ya utawala huo dhidi ya Katibu Mkuu wa harakati hiyo, Hassan Nasrullah, katika mashambulizi ya anga kwenye kitongoji cha kusini cha Beirut Ijumaa iliyopita.

Gazeti la New York Times limewanukuu maafisa wa serikali ya Washington wakisema kuwa Rais wa Marekani, Joe Biden, amemfahamisha Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kwamba mauaji ya Nasrullah huenda yakazusha vita vya kieneo, na kumtaka asimamishe moto wa vita.

342/