15 Februari 2021 - 06:53
Saudia yaendelea kufunga misikiti baada ya kesi ya COVID-19 kuongezeka

Misikiti mingine 8 imefungwa kwa muda maeneo mbali mbali ya Saudia kufuatia ongezeko la maambukizi ya COVID-19 nchini humo.

Shirika la habari la Ahlubayt (as)ABNA: Misikiti huyo imefungwa Ijumaa kufuatia amri ya Wizara ya Masuala ya Kiislamu huku maimamu wa misikiti wakitoa wito kwa Waislamu kuchukua tahadhari za kuzuia kuenea Corona na kusisitiza kuwa kufanya hivyo ni wajibu wa kidini na kitaifa.

Katika kipindi cha wiki moja iliyopita, jumla ya misikiti 52 imefungwa kote Saudia baada ya kubainika kuwepo maambukizi ya Corona miongoni mwa waliosali katika misikiti hiyo.

Wizara ya Masuala ya Kiislamu Saudia imeimarisha oparesheni ya kuchunguza misikiti yote nchini humo ili kuzuia maambukizi ya Corona. Wasimamizi wa misikiti wanashirikiana na maafisa wa usalama na mashirika yasiyo ya kiserikali ili kuhakikisha kuwa ugonjwa wa Corona hausambazwi misikitini.

Hadi sasa watu 372,000 wameambukizwa Corona Saudi Arabia na miongoni mwao 6,429 wamepoteza maisha.

342/