Katika ujumbe kwa Kamanda wa Jeshi la Majini la Iran kwa mnasaba wa Luteka ya Saba ya Pamoja ya Ukanda wa Usalama wa Baharini 2025, Araghchi ameeleza bayana kuwa, usalama na maendeleo ya msingi wa baharini yanahitaji uwepo wa nguvu katika eneo pana la bahari.
Mwanadiplomasia huyo mkuu wa Iran ameeleza azma ya Jamhuri ya Kiislamu ya kudumisha na kuimarisha usalama wa Ghuba ya Uajemi, Lango-Bahari la Kistratijia la Hormuz, Bahari ya Oman na kwingineko, na amesisitiza kwamba maneva ya hivi sasa yatadhihirisha azma hiyo mbele ya waangalizi wa kimataifa.
Mazoezi haya yaliyoanza Jumatatu ya Machi 10 na kuzinduliwa rasmi jana Jumanne, yanahusisha vikosi vya majini vya Iran, Russia na China, pamoja na waangalizi kutoka nchi za Jamhuri ya Azerbaijan, Afrika Kusini, Oman, Kazakhstan, Pakistan, Qatar, Iraq, Umoja wa Falme za Kiarabu, na Sri Lanka.
Meli za Jeshi la Majini la Iran na Kikosi cha Majini cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) pia zinashiriki katika mazoezi hayo.
Lengo kuu la mazoezi haya ni kuboresha usalama wa majini na ushirikiano endelevu wa safari za baharini katika eneo la Kaskazini mwa Bahari ya Hindi.
Aidha, mazoezi haya yanalenga kuonyesha uwezo wa vikosi vya majini vya Iran kimataifa, kuimarisha uwezo wao wa kitaalamu katika mafunzo ya kijeshi ya pamoja na kuendeleza diplomasia ya baharini ya Jamhuri ya Kiislamu.
342/
Your Comment