Rais wa Ufaransa amefanya safari kwenda Urusi kujadili kuhusu njia za kumaliza mgogoro wa Ukraine kwa njia ya mazungumzo na amani, Francois Hollande amekuwa kiongozi wa kwanza wa Ulaya kwenda Urusi kufanya mazungumzo Vladimir Putin kuhusiana na Ukraine.
Wakati huo huo serikali mjini Kiev imetangaza duru mpya ya mazungumzo ya amani wiki ijayo.
Mkutano kati ya Hollande na Putin katika eneo la kidiplomasia katika uwanja wa ndege nje ya mji mkuu wa nchi hiyo , umekuja wakati mzozo katika eneo la mashariki mwa Ukraine umeporomosha uhusiano kati ya mataifa ya magharibi na Urusi na kuwa katika kiwango chake cha chini kabisa tangu wakati wa baada ya vita baridi.
Kiongozi huyo wa Ufaransa amesema ana matumaini ya kuzuwia mtengano mwingine wa mataifa ya magharibi na mashariki na kwamba anamatumaini kuona "matokeo mazuri " kutoka katika mazungumzo hayo na Putin, ambaye mataifa ya Ulaya na Marekani yanamshutumu kwa kuwapa silaha na fedha waasi mashariki mwa Ukraine.
Rais wa Ufaransa amesema"Kuna wakati ambapo tunahitaji kutumia fursa. Huu ndio wakati.. nafikiri tunapaswa kuzuia kuta nyingine kututenganisha,"
pia amezungumza na rais wa Ukraine Petro Poroshenko mapema jana.
"Tunapaswa kutafuta suluhisho kwa pamoja," Francois Hollande amemwambia Vladimir Putin kiongozi wa Urusi, ambaye wiki hii ametoa hotuba ya nzito akiyashutumu mataifa ya magharibi kwa kuikandamiza Urusi.
Putin amesema kuna "matatizo magumu" kuyashughulikia lakini ziara hiyo , bila shaka itachangia katika suluhisho la matatizo mengi." Katika hatua muhimu ya kukiri, Putin amesema kwa mara ya kwanza kwamba waasi wanaoiunga mkono Urusi wamekiuka makubaliano tete ya kusitisha mapigano na Ukraine.
"Tunaona kwamba pande zote mbili viongozi wa Ukraine na upande wa viongozi wa Donetsk na Lugansk , kwa pande zote , si kila kitu ambacho kimeheshimiwa," Vladimir Putin amewaambia waandishi habari baada ya mkutano ambao umechukua karibu masaa mawili.
Ziara ya dakika za mwisho ya Hollande, ambayo chanzo kimoja katika ujumbe wake kimesema pia ilikubaliwa na kansela wa Ujerumani Angela Merkel, imekuja wakati Ukraine imetangaza duru mpya ya mazungumzo na waasi mjini Minsk wiki ijayo kujaribu kuokoa makubaliano ya mwezi Septemba yaliyovurugika ya kusitisha mapigano.
Mazungumzo hayo yatafanyika siku ya Jumanne, pia tarehe hiyo imepangwa na pande zote kwa ajili ya kupatikana makubaliano mapya ya kusitisha mapigano.
Ukraine na waasi, ambao mapigano yao upande wa mashariki mwa nchi hiyo yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 4,300, wamekubaliana kusitisha operesheni zao Desemba 9, na kuiita siku ya "ukimya".
"Katika muda wa siku 30, pande hizo mbili zitawajibika kurejesha nyuma silaha zao nzito kutoka katika eneo lisilotakiwa kuwa na mapambano ya silaha lililoainishwa katika rasimu ya Minsk," Poroshenko amesema. Kiongozi huyo wa Ukraine pia amesema kwamba pande zitakazokutana katika mji mkuu wa Belarus zitalenga katika "kuthibitisha muda maalum uliopangwa kutekeleza makubaliano ya mwanzo ya Minsk."
Makubaliano ya mwanzo yalizitaka pande zote kuacha kushambulia na kuondoa silaha na majeshi yao, lakini yalifanikiwa tu kuzuwia ghasia mbaya kutokea bila ya kusitisha machafuko kabisa.