Main Title

source :
Ijumaa

27 Septemba 2013

20:30:00
467647

HEKAYA

HEKAYA YA MZEE NA NYOKA

Mzee mmoja aliazimia safari kuelekea mashariki ya mbali, hivyo alifungasha mizigo na kupanda Ngamia wake na kuanza safari.Njiani alifika sehemu kwenye mti mkubwa ambapo aghalabu wasafiri hupumzikia hapo.

Lakini kabla ya mzee huyo kufika hapo  wasafiri walikuwa wamepumzika sehemu hiyo na kuondoka, hivyo walishau kuzima moto walokuwa wakiutumia ,kwabahati mbaya upepo  ulivuma nakupelekea moto huo kuunguza sehemu kubwa ya mwitu huo.

Mzee alipokuwa akitazama tukio hilo, ghafla akashituka na kusema hammadi! Kwani aliona nyoka akiwa katikati ya moto na imebakia kidogo tu moto umuangamize.

Mzee aliingiwa na huruma na kuwaza:”ingawa nyoka ni adui yangu lakini sidhani kama ni vibaya kumsaidia “hivyo alichukua  mfuko na kuufunga kwenye ncha ya mwanzi na kumnyooshea nyoka huyo ilikumnusuru, basi Nyoka aliingia kwenye mfuko na kujiviringisha ndani yake, na mzee yule akamuokowa kwa kumrusha nje ya moto ule, na hapo ukatimia muradi wa bwana huyo  wa kumnusuru nyoka yule .

   Nyoka alipotoka kwenye mfuko, alimgeukia mzee na kumwambia” ijapokuwa umeniokoa lakini mimi ni hasimu wa mwanadamu na uhasimu wetu ni wamiaka dahari, hivyo sitaondoka mpaka nihakikishe nimekuuwa”.

Mzee alihamaki  na kusema”je? Hayo ndio malipo ya hisani nilokufanyia basi kwanini umlipe ubaya alokufanyia hisani?”

Nyoka akasema:”kulipa mabaya kwa aliyekufanyia hisani si nuksani, na kama haujaridhia uamuzi wangu twaweza kusaili walimwengu kabla sijakuuwa”.

Ndipo walipomwona Ng’ombe akiwa machungani wakamwita na kumsaili: je Kunaulazima malipo ya hisani yawe hisani? .

Ng’ombe akajibu akisema: ndio! lakini  Mwanadamu hajui ihsani, kwani nilikuwa nimefugwa na mtu mmoja na alikuwa akijifaharisha sana nami, kwasababu nilikuwa nikimzalia ndama takribani kila mwaka, ambapo walikuwa wakinywa maziwa yangu na kuyauza, na hivisasa nimezeeka siwezi tena kuzaa. Anaenifuga alipoona nimenona na kupendeza aliniuza ili wanichinje na kunufaika kwa nyama na ngozi yangu, je,haya yanafaa kuwa ni malipo ya wema na hisani zote nilizowafanyia?

Nyoka akasema: mzee umemsikia Ng’ombe?

Mzee alilia hali akisema :chonde usihukumu kwa ushahidi mmoja.

Nyoka akatupa jicho kwa mti na kukata shauri wauulize mti pia , walipouliza mti, mti ulisema:”kwa kawaida malipo ya hisani huwa ni hisani ila kwa wanadamu nikinyume chake”kwani mimi ni mti mkubwa na kwa muda mrefu nipo hapa mwituni, mara kwa mara wasafiri hukaa na kupumzika chini ya kivuli changu, cha ajabu mara utamsikia mmoja wao akisema:”tawi hili linafaaa kwa kutengenezea upinde, na mwingine husema:mbao za mti huu ni imara na ninzuri kwa vitanda hata milango “baada ya hapo wakaja na mashoka, mapanga na misumeno na kukata sehemu kubwa ya mwili wangu,”Je haya ndio malipo ya kivuli na upepo mwanana nilowapatia?”

Nyoka akasema: mzee nadhani umefika muda wa mimi kutekeleza azma yangu.

Mzee akambembeleza nyoka akisema: tafadhali nahitaji shahidi mwingine ili niwe radhi na hukumu.

Kumbe katika kipindi chote hicho Sungura alikuwa amejificha na kushuhudia tukio lote, ndipo alipojitokeza, Nyoka alipomwona Sungura akasema sasa tumuulize Sungura!

Mzee akamwuliza Sungura: Je ni laiki kumlipa ubaya alokufanyia hisani?

Sungura  akasema: Kwani wewe umemfanyia hisani gani nyoka huyu hata useme hivyo?

Mzee akajibu: nimemwokoa kwenye moto.

Sungura akasema:”acha maskhara mzee! Umeweza vipi kumuokoa nyoka kwenye moto huu”

Mzee akasema: sadiki nisemayo! Nilifunga mfuko kwenye ncha ya mwanzi ndipo nyoka alipoigia mfukoni na hatimaye nikamuokoa na moto huu.

Sungura akasema: nastajabu! Imewezekana vipi joka hili likaingia kwenye kifuko hiki? alakulihali  ilinisadiki usemayo, basi nyoka aingie tena kwenye mfuko huu ili niweze toa hukumu iliyo sahihi.

Nyoka akahadaika na maneno ya Sungura na akaingia kwenye mfuko, ndipo Sungura alipomwambia mzee:”usipoteze muda muue kabla haja kuuwa”.

Mzee alitumia vizuri fursa hiyo na kumuua nyoka.

Mpenzi msomaji, mwenye akili timamu hatakiwi kusahau uhasimu uliopo baina yake na adui yake, hususan uadui uliopo baina ya mwanadamu na shetani rajimi, ambaye amekula kiapo kuwa atatumia hila zake zote, kuhakikisha anawapoteza wana wa Adamu  na kuwaingiza Jahanamu. 

 Kisa hiki pia utakipata katika site ya www.Tafakuri.com