5 Novemba 2025 - 14:39
Source: Parstoday
Utafiti: Vita vya mauaji ya kimbari vya Israel vimegharimu zaidi ya miaka milioni 3 ya maisha ya mwanadamu huko Gaza

Utafiti wa hivi karibuni uliochapishwa katika jarida la Lancet umefichua kuwa zaidi ya miaka milioni tatu ya maisha ya binadamu yamepotea katika Ukanda wa Gaza tangu utawala ghasibu wa Israel uanzishe kampeni yake ya mauaji ya kimbari dhidi ya watu Ukanda wa Gaza ulio chini ya mzingiro, mwezi Oktoba mwaka 2023.

Waandishi wa utafiti huo kwa majina ya Sammy Zahran wa Chuo Kikuu cha Umma cha Colorado na Ghassan Abi-Sittah wa Chuo Kikuu cha Kimarekani cha Beirut, Lebanon wamesema kuwa raia wamepoteza maisha ya kuishi kwa miaka kadhaa na kwamba zaidi ya miaka milioni moja ya maisha inayojumuisha watoto chini ya umri wa miaka 15 imepotea.

Neno "miaka ya maisha iliyopotea" linamaanisha jumla ya miaka ya maisha inayotarajiwa ambayo Wapalestina waliouawa wangeishi kama wasingekufa mapema.

Watafiti hao wameeleza kuwa hesabu hiyo inajumuisha vifo vya moja kwa moja kutokana na mashambulizi ya Israel, ukiondoa wale walioaga dunia kutokana na miundombinu iliyoharibiwa, njaa, upungufu wa maji mwilini, magonjwa na kusambaratika kwa mfumo wa matibabu wa Gaza.

Utafiti wa awali wa Lancet ulifichua kwamba idadi ya vifo iliyoripotiwa huko Gaza ni ndogo sana, ikikadiria idadi halisi ya vifo vya watu wa Gaza kuwa kwa uchache ilikuwa asilimia 40 zaidi kuliko ile iliyorekodiwa rasmi.

Jarida hilo la masuala ya afya limeongeza kubainisha kuwa ikiwa hesabu zinajumuisha vifo visivyo vya moja kwa moja,  ikiwa ni pamoja na vile vilivyosababishwa na kuzorota kwa vituo vya afya, njaa na magonjwa basi Wapalestina waliouawa wanaweza kuwa kati ya 149,000 na 598,000.

Utafiti huo uliochapishwa na jarida la masuala ya tiba la Lancet umetolewa wiki chache tu baada ya usitishaji vita huko Gaza kuanza kutekelezwa tarehe 10 Oktoba.

Your Comment

You are replying to: .
captcha