Takriban watu milioni moja wameandamana katika miji ya Brazil wakiipinga serikali ya Rais Dilma Rouseff wanayemshutumu kwa masaibu ya uchumi kudorora, kupanda kwa gharama ya maisha na ufisadi. Waandamanaji hao wanamtaka Rouseff wa chama cha mrengo wa kushoto kushitakiwa kwa kutumia madaraka vibaya. Maandamano hayo yaliyofanyika hapo jana kote nchini Brazil yanakuja wakati ambapo nchi hiyo inakabiliwa na mgogoro wa kiuchumi ambao umekuwepo tangu Rouseff kuingia madarakani mwaka 2011. Rousseff ambaye anahudumu kipindi cha pili madarakani hatarajiwi kuondolewa madarakani licha ya maandamano hayo makubwa.Waandamanaji wameghadhabishwa na kashfa kubwa ya ufisadi katika shirika la mafuta la Petrobas ambayo wanamshutumu rais huyo kwa kutochukua hatua muafaka kuukabili ufisadi. Maandamano makubwa zaidi yalishuhudiwa katika mji wa Sao Paulo ambao ni ngome ya upinzani.