Jeshi la anga la Kenya (KDF) limezishambulia kambi mbili za al Shabaab nchini Somalia leo hii. Chanzo kutoka katika jeshi hilo kimesema hilo ni shambulio la kwanza kubwa baada ya shambulizi la wiki iliyopita la wanamgambo wa kundi hilo katika chuo kikuu cha Kenya. Ndege za kivita zilishambulia kambi hizo zilizopo Gondodowe na Ismail, zote zikiwa katika jimbo la Gedo, lililopo mpakani mwa Somalia na Kenya. Chanzo hicho kiliendelea kusema kutanda kwa kiwango kikubwa cha moshi angani kumefanya iwe vigumu kuweza kutambua athari za mashambulizi katika maeneo hayo ya kambi. Aidha afisa huyo wa KDF alisema waliyalenga maeneo hayo mawili kutokana na kupata taarifa kuwa wafuasi wa al-Shabaab wanaoishambulia Kenya wanatokea katika kambi kambi hizo. Afisa huyo wa jeshi aliyesamema hayo akitolea mfano shambulizi lililosababisha mauwaji makubwa katika Chuo Kikuu mjini Garisa, kilichopo umbali wa kilometa 200 kutoka mpakani mwa Somalia.