28 Januari 2023 - 18:07
Ayatullah Issa Qassim ayataka mataifa ya dunia yaache kuwakingia kifua maadui wa Uislamu

Ayatullah Issa Qassim, kiongozi wa Waislamu wa Madhehebu ya Shia nchini Bahrain amezitaka serikali na tawala za mataifa ya dunia kuacha kuwaunga mkono na kuwakingia kifua watu ambao wana uadui na Uislamu.

Katika ujumbe wake huo ulioandikwa katika ukurasa wa Harakati ya al-Wifaq wa mtandao wa kijamii wa twitter, kiongozi huyo wa kimaanawi wa Bahrain amesisitiza kuwa, tawala na serikali mbalimbali duniani zinapaswa kuwa na ghera na heshima kwa Qur'ani Tukufu na matukufu ya dini za wengine..

Katika sehemu nyingine ya ujumbe wake huo, Sheikh Issa Qassim ameziasa tawala na serikali mbalimbali duniani na kuzitaka zisishirikiane na maadui wa Uislamu kama ambavyo zinapaswa kulaani kitendo cha watu kuchoma moto Qur'ani Tukufu.

Msomi huyo mashuhuri wa Kishia wa Bahrain ameendelea kusisitiza kwamba matusi, uwongo, kashfa, unafiki na kuvunjiwa heshima maadili matukufu hakuwezi kwa vyovyote vile kuchukuliwa kuwa ni uhuru wa maoni. 

Jumapili iliyopita, Edwin Wagensveld, mwanasiasa wa siasa kali za mrengo wa kulia wa Uholanzi, na kiongozi wa kundi la chuki dhidi ya Uislamu la Pegida, alirarua kurasa za Qur’ani Tukufu  huko The Hague, mji mkuu wa Uholanzi. Video ya Wagensveld kwenye Twitter imeonyesha kuwa alichoma kurasa zilizochanwa za Qur’ani Tukufu.

Uchochezi huo mpya ulifuatia kitendo sawa na hicho cha chuki dhidi ya Uislamu siku ya Jumamosi nchini Sweden Rasmus Paludan mwenye msimamo mkali  alichoma nakala ya Qur’ani Tukufu mbele ya ubalozi wa Uturuki mjini Stockholm, kitendo ambacho kiliidhinishwa na kusimamiwa na polisi nchini humo na kuhakikisha kinafanyika kama ilivyopangwa.

342/