13 Julai 2012 - 19:30

Wakati hayo yakiendelea, mkuu wa majeshi wa Iran, Jenerali Hassan Firouzabadi, amezituhumu Uturuki na Jordan kwa kuwaruhusu waasi wa Syria kuishambulia nchi hiyo kupitia mipakani mwao.

Akinukuliwa na shirika la habari la ISNA, Jenerali Firouzabadi amesema kwamba ni jukumu la majirani wa Kiislamu wa Syria kujizuia kuwaunga mkono magaidi na akazitaka nchi hizo kufunga mipaka yake.

Upinzani nchini Syria na mataifa ya Magharibi wanailaumu Iran kwa kuipa silaha serikali ya Syria, lakini naibu waziri wa mambo ya nje wa Iran, Hossein Amir Abdolahian, amesema makundi ya kigaidi yanayoendesha mauaji nchini syria yanapata msaada kutoka mataifa ya jirani, na kwamba tayari nchi yake imeshamfahamisha hilo, mjumbe maalum wa kimataifa kwa Syria, Koffi Annan.

Tangu maandamano yaanze nchini Syria miezi 16 iliyopita, zaidi ya watu 17,000 wanaripotiwa kupoteza maisha yao, wengi wao wakiwa wanawake na watoto.