9 Mei 2023 - 14:26
Mahathir Muhammad: Washington inaisukuma dunia katika vita vya tatu vya dunia

Waziri Mkuu wa zamani wa Malaysia, Mahathir Mohamad amesema kuwa serikali ya Marekani inawasukuma wanaadamu kwenye vita vya dunia kwa kuchangia kuibuka kwa kambi mbili hasimu.

Mahathir, 97, amesema katika mahojiano na gazeti la Uchina, Global Times kwamba: "Marekani itajaribu kuzishawishi nchi zingine kujiunga na vita dhidi ya Russia, na Russia kwa upande wake italazimika kutafuta nchi marafiki kuiunga mkono."

Mahathir Mohamad ameongeza kuwa, kutakuwapo makabiliano kati ya kambi ya Mashariki na kambi ya Magharibi, na suala hili litashadidi na hatimaye kuwa vita vya dunia.

Waziri Mkuu wa zamani wa Malaysia amesema, mgogoro wa Ukraine ambao ulichochewa na nchi za Magharibi, tayari umeathiri dunia nzima, na  kuongeza kuwa hali hiyo tata imesababisha kuongezeka kwa gharama za bidhaa za kimsingi kote duniani, suala ambalo pia limeathiri vibaya usafirishaji wa nafaka.

Amesema kuwa wito wa Ukraine kujiunga na NATO ni uchochezi, na kuongeza kuwa" "Iwapo Ukraine haitajiunga na NATO, Russia haitahisi tishio kubwa na hakutakuwapo makabiliano, lakini mchakato huo utakapoanza, Moscow itachukua hatua kali."

Ameongeza kusema kuwa nchi wanachama wa NATO hazishiriki moja kwa moja katika mzozo wa Russia na Ukraine, kwa sababu Ukraine sio mwanachama wa muungano huo; hata hivyo, makabiliano ya nchi za Magharibi na Russia yanazidhuru sana nchi wanachama wa NATO.

Mahathir Mohamad amezishauri Russia na Ukraine kuingia kwenye mazungumzo ya moja kwa moja kwa ajili ya kupata suluhisho la mgogoro wa sasa.

342/