12 Agosti 2025 - 22:16
Wapenzi wa Imam Hussein (as) 36,000 wa Gilan Wajiandikisha kwa ajili ya Arubaini / Waanza Kurudi Nyumbani Taratibu

Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Arubaini mkoa wa Gilan ametangaza kuanza kwa kurejea taratibu kwa mahujaji wa Arubaini mkoani humo na kusema kuwa hadi sasa zaidi ya watu 36,000 kutoka Gilan wamejiandikisha kwenye mfumo wa Samah ili kushiriki katika maadhimisho ya kimataifa ya Arubaini ya Imam Husein (a.s).

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Ali Baqeri, Naibu Gavana wa Gilan anayehusika na masuala ya kisiasa, kiusalama na kijamii na pia Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Arubaini ya mkoa, leo Jumanne tarehe 12 Agosti, 2025, amesema kuwa usafirishaji wa Mahujaji (Mazuwwari) unafanywa kwa mabasi ya usafiri wa umma, treni, na safari maalum za ndege kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Rasht.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha tarehe: 05 hadi 11 Agosti, takribani Mahujaji / Mazuwwari 9,000 walisafirishwa kutoka Gilan kwenda mipakani mwa nchi kwa kutumia mabasi 300 ya umma katika safari 118 rasmi, na kwamba hadi sasa zaidi ya watu 3,000 wamerejea mkoani.

Baqeri amesema kuwa leo mabasi 20 yenye kubeba mahujaji 557 yameingia Gilan na pia mahujaji 865 waliokuwa wameondoka kwa treni wamewasili nyumbani.

Kuhusu usafiri wa anga, amesema jumla ya mahujaji waliotumia ndege katika safari za kwenda na kurudi imekuwa zaidi ya watu 4,000.

Amebainisha pia kuwa mwaka huu kulishuhudiwa ushiriki wa kipekee wa wafadhili, watumishi na wasimamizi wa mahema ya huduma (Mawakibu) kutoka Gilan, ambao wamekuwa miongoni mwa nguzo kuu za mafanikio ya maadhimisho haya makubwa ya kimataifa.

Kwa mujibu wake, kuna Mawakibu 32 yanayofanya kazi ndani ya Gilan, huku manne yakitoa huduma mipakani, na mengine mjini Najaf na Karbala yakitoa huduma za dharura na matibabu kwa kiwango cha juu. Huduma hizi nyingi zimekuwa zikitekelezwa kwa msaada na mchango wa wananchi na wafadhili.

Ametoa wito kwa mahujaji kuepuka kurudi nyumbani katika siku zenye msongamano mkubwa, na kwa wanaotumia magari binafsi kupumzika kwenye mahema ya huduma mipakani ili kulinda afya zao. Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha muhuri wa kuingia na kutoka unatiwa ipasavyo kwenye pasipoti.

Baqeri amehitimisha kwa kueleza kuwa vyombo vya usalama na polisi, kwa mshikamano wa hali ya juu, vinaendelea kutumia nguvu zote kuhakikisha usalama na ustawi wa mahujaji, na kwamba harakati za mahujaji zinaendelea kwa utaratibu.

Tags

Your Comment

You are replying to: .
captcha